NA RICHARD MUNGUTI
MAHAKAMA itaamua Ijumaa kuhusu ombi la Seneta wa Busia, Okiya Omtata, kumfunga Mkurugenzi wa Mamlaka ya Kudhibiti Kawi (EPRA), Bw Daniel Kiptoo, kwa kuikaidi.
Wakati huo huo, Jaji Mugure Thande ameongeza marufuku ya utekelezaji wa mapendekezo mapya kwenye Sheria ya Fedha 2023 hadi Jumatatu ijayo, Julai 10.
Baadhi ya mapendekezo hayo ni nyongeza ya mafuta kutoka asilimia nane hadi 16. Punde baadaye, Bw Kiptoo alitangaza bei mpya za mafuta.
Mnamo Jumatano, Bw Omtatah aliambia mahakama kuwa, Sheria ya Fedha 2023 haikujadiliwa na mabunge yote mawili, yaani Bunge la Kitaifa na Seneti.
“Wakenya hawastahili kulipa ushuru kwa vile Waziri wa Fedha aliwasilisha hoja ya matumizi ya Sh3.6 trilioni bila kuonyesha pesa hizo zitatolewa wapi,” Omtatah alisema akiongeza kuwa, Spika wa Bunge la Kitaifa na mwenzake wa Seneti walikula njama kupitisha sheria hiyo.
Aliiomba korti isitishe kutekelezwa kwa sheria hiyo ya fedha 2023 kwa vile itaumiza wananchi.
Wakili Otiende Amollo alisema sheria hiyo itawafanya Wakenya watumwa kwa vile wanatozwa kodi kinyume cha sheria.
Bw Amollo alieleza mahakama Wakenya hawastahili kutozwa ushuru kwa sababu Katiba imekiukwa.
“Kifungu nambari 203 cha Katiba kinakubalia bunge kuwatoza Wakenya ushuru baada ya mabunge yote mawili kujadiliana na kukubaliana,” akasema mbunge huyo wa Rarieda.
Alidai spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula na wa Seneti Amason Kingi walikubaliana kukaidi sheria kwa kutowasilisha mswada huo kwa bunge la Seneti kujadiliwa na kuidhinishwa.
Mawakili Githu Muigai na Kimani Kiragu walipinga kesi hiyo wakisema utoaji wa huduma umekwama.
Subscribe our newsletter to stay updated