Na ERIC MATARA
WAZIRI wa Elimu George Magoha ameshikilia kuwa mitihani ya kitaifa ambayo imeratibiwa kuanza Machi 2022, itaendelea jinsi ilivyopangwa.
Kauli yake inajiri wiki chache baada ya Mwenyekiti wa Muungano wa Walimu Wakuu wa Shule za Upili (KESSHA) Kahi Indimuli kupendekeza mitihani hiyo iahirishwe kutokana na migomo mingi inayoendelea kushuhudiwa.
Kando na Bw Indimuli, walimu wakuu wa shule mbalimbali walipendekeza KCSE na KCPE iahirishwe kama njia ya kuwatuliza wanafunzi wasishiriki migomo.
Hata hivyo, Profesa Magoha alisema kuwa mitihani hiyo itaendelea na hata kuwataka wazazi kuwashauri wana wao wazingatie mno nidhamu wakiwa nao wakati wa likizo fupi ya Krismasi na Mwaka Mpya.
“Mitihani iko tayari na hatutasongesha tarehe mbele. Hakuna haja ya watahiniwa waingiwe na taharuki ila wasalie watulivu na wawe tayari kufanya mtihani,” akasema Profesa Magoha.
Alisisitiza kuwa mitihani hiyo itazingatia sana hoja kuwa wanafunzi hawakuwa shuleni kwa muda mrefu kutokana na janga la virusi vya corona.