• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 6:09 PM
Mwalimu afariki siku chache kabla ya kuanza kazi aliyotafuta kwa muda

Mwalimu afariki siku chache kabla ya kuanza kazi aliyotafuta kwa muda

NA MWANGI MUIRURI

MWALIMU wa kiume aliyekuwa aanze kufundisha leo Septemba 1, 2023, katika shule ya Murang’a alipatikana ameuawa na kutupwa kwa mto.

Bw Andrew Njiru,35, alikuwa aanze kufunza katika Shule ya Msingi ya Rutune iliyoko katika eneobunge la Kiharu lakini mnamo Jumatano, mwili wake ukapatikana katika Mto Sagana.

Mkuu wa polisi wa Murang’a Mashariki Bi Mary Kasyoki amesema kwamba uchunguzi wa kubainisha kilichomuua Bw Njiru umeanzishwa.

Amesema kwamba mwili utafanyiwa upasuaji ili daktari aandae ripoti kuhusu nini hasa kilichomuua.

“Aidha, tutaandika taarifa kutoka kwa wote walio na habari kuhusu mazingira ya mauti haya. Mwishowe tutapata jibu na haki itendeke,” akasema.

Huku shughuli hiyo ikisubiriwa, babake mwalimu huyo, Bw William Mwangi, kwa upande wake amesema kwamba habari alizokusanya zinaonyesha mwanaye aliuawa.

“Nimedokezewa kwamba Bw Njiru aliyekuwa amekodisha chumba cha kupanga karibu na shule hiyo, alichanganyikiwa wakati stima ilipotea nchini mnamo Agosti 27, 2023,” akadai.

Ameongeza kwamba kijana wake alikuwa ameenda kwa duka kununua mshumaa lakini akachanganyikiwa kwani aliporejea, aliingia kwa majirani.

“Nimearifiwa kwamba alidhaniwa kuwa mwizi na ndugu wawili majirani wakamtandika hadi akafa na baadaye wakampakia ndani ya gari na wakatoweka na mwili wake,” akasimulia.

Amesema mtoto wake amekuwa akisaka ajira kwa miaka tisa na mara hii fursa ilikuwa imepatikana lakini ikakatika ghafla.

  • Tags

You can share this post!

Dhambi za zamani: Kidero ashtakiwa kwa ufujaji pesa miaka 9...

Tumeweka WiFi mpate kazi za kidijitali, serikali yaambia...

T L