NA SAMMY KIMATU
WAANDAMANAJI waliokusanyika karibu na jumba la Nation Centre wakiimba nyimbo za kuilaani serikali huku wakiwa wamebeba mabango wametawanywa na maafisa wa polisi wa kupambana na ghasia.
Katika kukurukaka za kutoroka, polisi waliwakamata watu watatu, mwanamume na wanawake wawili, katika barabara ya Banda.
Waandishi wa habari waliowaona maafisa wakiwakanyaga wanawake hao kifuani, tumboni, na miguuni wamelaani unyama huo kwa kupiga kelele. Maafisa walitumia njumu zao kutekeleza unyama huo.
Taifa Leo imehesabu magari saba ya polisi katika eneo la kisa yakiwemo yale yaliyo na nambari za usajili za serikali na mengine yenye nambari za usajili za kawaida.
Tukio hilo limewalazimisha waliokuwa wamefungua maduka ya biashara kuyafunga haraka.
Ilibidi waumini wa dini ya Kiislamu waliokuwa wakitembea kuelekea kwenye msikiti wa Jamia kwa swala ya Ijumaa kuchukua tahadhari zaidi na hata wakati mwingine kukimbia kuepuka kadhia ya maafisa hao ambao hawakuonyesha huruma kwa yeyote.