NA CHARLES WASONGA
WAKENYA wanaotaka kupata kitambulisho kipya cha kitaifa sasa watahitajika kulipa Sh300 na wala si Sh1,000 jinsi ilivyotangazwa awali na serikali.
Hii ni kulingana na mwongozo mpya wa ada zinazotozwa huduma za kimsingi na Idara ya Uhamiaji na Huduma za Raia ambao ulitolewa na Waziri wa Usalama wa Ndani Kithure Kindiki mnamo Jumanne jioni.
Profesa Kindiki alitoa mwongozo huo baada ya kufutilia mbali notisi ya awali iliyoongeza ada ya kuchukua vitambulisho vya kitaifa kutoka Sh100 hadi Sh1,000, ili kutoa nafasi kwa ushirikishaji wa maoni kutoka kwa umma.
Wakenya maskini hohehahe, wakiwemo mayatima na wale ambao wataonyesha kuwa hawawezi kulipa Sh300 kupata stakabadhi hizo, watalipiwa ada hizo na serikali.