• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 7:50 AM
Wanaokataa kulipa mkopo wa Hasla kujuta

Wanaokataa kulipa mkopo wa Hasla kujuta

NA JOSEPH OPENDA

WAKENYA ambao walikopa pesa za Hazina ya Hasla na wameshindwa kulipa, hawataruhusiwa kupokea mkopo wa hazina hiyo utakaotolewa kwa makundi ili kuwakwamua kibiashara.

Kwa mujibu wa Rais William Ruto, Wakenya hao watalazimika kulipa madeni wanayodaiwa na hazina hiyo kabla ya kupokezwa mkopo utakaotolewa kwa makundi ya kibiashara.

Kulingana na takwimu zilizotolewa na serikali, asilimia 29 ya Wakenya ambao walichukua mkopo wa Hazina ya Hasla hawajaulipa.

Hali hii imeibua wasiwasi kuwa idadi kubwa ya Wakenya watakuwa wakiendelea kukopa pesa hizo bila ya kuzilipa.

Rais alifichua kuwa serikali imeongeza Sh10 bilioni zaidi katika hazina hiyo lakini kwenye kitengo kinachojihusisha na biashara.

Alisikitika kuwa japo kuna Wakenya ambao wamelipa mkopo wao, wapo wengine ambao walikopa na hawajaonyesha nia ya kuulipa.

“Nafahamu kuwa kuna asilimia kubwa ya Wakenya ambao hawajalipa mkopo wao ila nataka kuwaambia kuwa hawataenda mbali. Tumeongeza pesa ambazo zimetengewa kitengo cha fedha ila hawatapata mkopo huo hadi wakamilishe deni lao,” akasema Rais Ruto.

Kiongozi wa nchi alikuwa akizungumza akiwa katika eneobunge la Rongai, Nakuru wakati wa kutoa vyeti 1,900 vya ardhi katika maeneo ya Majani Mingi na Lomollo.

Pia Rais alisema kuwa serikali yake imetoa Wakenya wote ambao majina yao yalikuwa kwenye Mashirika ya Kufuatilia Madeni (CRB).

“Tumewaongezea Sh10 bilioni za kibiashara. Makundi yatakuwa yakipata kati ya Sh20,000 na Sh1 milioni ila kabla upate hiyo milioni, lazima ulipe hela ambazo ulikuwa umekopa,” akaongeza Rais.

Kulingana na takwimu zilizotolewa na Waziri Simon Chelugui mnamo Julai 16, serikali ilikuwa imetoa Sh33 bilioni kama mikopo kwa watu binafsi.

Kati ya pesa hizo, Sh22 milioni zilikuwa zimerejeshwa huku Sh1.6 milioni zikielekezwa kwenye akiba ya waliokuwa wamekopa na kulipa mikopo yao.

Jijini Nakuru, zaidi ya asilimia 77 ya watu 878,000 ambao walikopa pesa za hasla wamelipa huku asilimia 23 wakikosa kutimiza wajibu huo. Kaunti hiyo ilipokezwa Sh2 bilioni za pesa za hazina hiyo.

Makundi yanayopokea mikopo ya hasla yatakuwa na watu 10 au zaidi na wataruhusiwa kupata mkopo wa kati ya Sh20,000 hadi Sh1 milioni huku wakitozwa riba ya asilimia saba.

Muda wa kulipa mkopo huo ni miezi sita ila wanaokopa wana nafasi ya kuanza kulipa pole pole au hata mara moja.

  • Tags

You can share this post!

Kesi dhidi ya Babu Owino yakosa kuendelea

Nyayo House kuna maradhi ya ufisadi, akiri Kindiki

T L