NA MERCY KOSKEI
WAZIRI wa Usalama wa Ndani, Kithure Kindiki ameuonya muungano wa Azimio la Umoja, kuhusu tishio la kuandaa maandamano kupinga matokeo ya kura kupitisha Mswada wa Fedha 2023.
Akionekana kulenga kinara wa Azimio, Bw Raila Odinga, Prof Kindiki alisema Jumapili, Juni 11, 2023 upande utakaoshindwa bungeni lazima uheshimu matokeo.
Waziri Kindiki alitoa onyo hilo, kufuatia tangazo la Bw Odinga kuwa endapo mswada huo tata unaopendekeza nyongeza ya ushuru (VAT) kwa bidhaa muhimu za kimsingi utapitishwa, Azimio haitakuwa na budi ila kurejelea mahandamano.
Akizungumza katika Kanisa la Methodist la Marimanti, Kaunti ya Tharaka Nithi, Prof Kindiki alimtaka Odinga kutumia mbinu zilizowekwa kisheria kuangazia malalamishi, badala ya kile alihoji kama ‘kushawishi umma kuandamana’.
“Serikali haitaruhusu machafuko ya aina yoyote kwa sababu ya maandamano, kama tuliyoshuhudia Februari 2023,” Waziri Kindiki alionya.
“Hatutaitikia watu wabinfasi kuvuruga biashara, kusimamisha usafiri na kuharibu mali.”
Azimio pia imetishia kurejelea maandamano baada ya mazungumzo ya mapatano kati yake na serikali ya Kenya Kwanza kugonga mwamba.