NA SAM KIPLAGAT
WAZIRI wa Mazingira na Misitu Soipan Tuya amewasilisha kesi mahakamani akitaka ulinzi dhidi ya mumewe, akidai yeye pamoja na wanawe wamekuwa wakiishi kwa hofu ya kushambuliwa mara kwa mara.
Kwenye kesi ambayo imetajwa katika Mahakama ya Watoto jijini Nairobi leo Jumatano asubuhi, waziri Tuya pia ameomba mahakama imuamuru Stephen Kudate kutoa Sh425,000 za karo ya watoto, matunzo na burudani.
Bi Tuya kwenye stakabadhi zilizowasilishwa mahakamani anadai kwamba mume wake huyo huwachukulia wanawe kama wafanyakazi wa nyumbani na amewadhulumu kisaikolojia, kihisia na hata kuwakaripia yeye waziri, wanawe na wafanyakazi wa nyumbani.
Amesema hali hii ya hofu imefanya aripoti matukio hayo katika kituo cha polisi cha Hardy.
“Hivyo mlalamishi ana hofu kwamba vipigo na dhuluma, kudhalilishwa, kudunishwa, vitisho na kuhangaishwa vimezidi dhidi yake, wafanyakazi wa nyumbani na watoto ambao kwa sasa wanaishi kwa hofu kuu,” anasema mlalamishi.
Akijibu, mshtakiwa ameiomba mahakama kushurutisha kila upande kutoa hati za kiapo kufichua utajiri, kipato, huku uamuzi ukisubiriwa. Mahakama imekubali ombi hilo na ikaagiza kesi kusikilizwa mnamo Novemba 13, 2023.