• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 7:55 AM
Ulawiti: Papa Francis asema viongozi wa kidini wahitaji kipindi kirefu cha utakaso

Ulawiti: Papa Francis asema viongozi wa kidini wahitaji kipindi kirefu cha utakaso

NA MASHIRIKA

VATICAN CITY

KIONGOZI wa Kanisa Katoliki Duniani Papa Francis mnamo Jumatano alisema kanisa hilo linahitaji kujitakasa kwa kipindi kirefu kutokana na kitendo cha viongozi wa kidini kuwanyanyasa vijana kingono.

Papa Francis alisema kuna umuhimu wa “kujitakasa kwa unyenyekevu na kwa muda mrefu” ili kukabiliana na “kilio cha uchungu” cha waathirika wa unyanyasaji wa kingono waliotendewa na viongozi hao.

Papa Francis alisema hayo katika mkutano wa faragha kati yake na waathirika hao.

Alikuwa katika ziara yake ya kwanza nchini Ureno.

Francis alikuwa akizungumza jijini Lisbon mwanzoni mwa ziara ya siku tano nchini humo.

Anatumai katika ziara yake, atawahamasisha vijana wa Kikatoliki wakati wa siku ya vijana duniani, tamasha kubwa zaidi la Kikatoliki duniani.

Miezi sita iliyopita, ripoti ya tume ya Ureno ilisema takriban watoto 4,815 walinyanyaswa kingono na viongozi wa kidini kwa zaidi ya miongo saba.

“Mzozo huu unatuomba kujitakasa kwa unyenyekevu kwa muda mrefu, tukianza na kilio cha uchungu cha waathirika, ambao lazima wakubaliwe na wasikilizwe kila mara,” Francis alisema katika hotuba yake kwa maaskofu, mapadre na watawa katika ibada ya jioni ndani ya makazi ya watawa.

Francis alikutana kwa faragha na waathirika 13 walionyanyaswa kingono katika ubalozi wa Vatican mjini Lisbon jana Jumatano jioni.

Vatican ilisema katika taarifa kwamba mkutano huo ulifanyika katika “mazingira ya usikilizaji mkubwa” na ulidumu kwa zaidi ya saa moja.

  • Tags

You can share this post!

Wafanyakazi kuanza kukatwa ushuru wa nyumba

Washukiwa 11 wafumaniwa wakikata magari ya serikali

T L