• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 8:55 PM
Wanafunzi 26 wateketea madarasa yaliposhika moto

Wanafunzi 26 wateketea madarasa yaliposhika moto

Na AFP

WATOTO 26 wenye umri wa kati ya miaka mitano na sita waliteketea hadi kufa madarasa yao yenye kuta za mbao yaliposhika moto Jumatatu jioni katika shule moja kusini mwa Niger.

Mkasa huo umetokea miezi saba baada mwingine kama huo kutokea katika jiji kuu Niamey.“Wakati huu, watoto 26 wamefariki na 13 wamejeruhiwa, nne kati yao wakiwa na majeraha mabaya zaidi,” akasema Chaibou Aboubacar, Meja wa jiji la Maradi.

Niger ambayo ni mmoja ya mataifa maskini zaidi ulimwenguni, imejaribu kusuluhisha shida ya uhaba wa madarasa kwa kujenga vibanda vya mbao na miti ili vitumike kama madarasa. Nyakati zingine watoto huketi sakafuni kwa kukosa madawati.

Mikasa ya moto hutokea katika madarasa aina hiyo lakini huwa hayasababishi maafa. Kufuatia kisa hicho cha Jumatatu, utawala wa eneo la Maradi umetangaza siku tatu ya maombolezo, kuanzia jana Jumanne.

Watoto 25 waliteketea hadi kufa baada ya moto kutokea katika shule moja katika kitongoji wanakoishi watu wa mapato ya kadri jijini Niamey mnamo Aprili mwaka huu.“Mkasa huu wa Jumatatu kwa mara nyingine, umewaweka raia wa Niger katika hali ya maombolezo,” serikali ikasema kwenye taarifa.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa kuanzia sasa serikali itapiga marufuku madarasa ambayo kuta zao zimejengwa kwa mbao na miti kote nchini humo.Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Nchini (NTU) Issoufou Arzika aliambia shirika la habari la AFP alisema moto huo wa Jumatatu “ulimaliza kabisa” shule hiyo iliyoko Maradi.

Arzika alisema chama chake kilikuwa kimewajulisha maafisa kuhusu hatari ya madarasa yaliyotengenezwa kwa mbao, baada ya mkasa wa moto jijini Niamey.“Ni sawa kuendesha masomo chini ya miti badala ya ndani ya vibanda vilivyojengwa kwa mbao miti na nyasi ambayo hushika moto kwa haraka.

Hii inahatarisha maisha ya wanafunzi,” akasema.Juzi Rais Mohamed Bazoum aliahidi kuondoa madarasa hayo ya mbao na kujenga yale ya mawe na saruji.Wakati huo huo, watu wawili wamefariki na wengine wengine wakajeruhiwa vibaya katika ajali ya barabarani iliyotokea katika barabara kuu nchini Sudan Kusini.

Barabara hiyo huunganisha nchi na eneo zima la Afrika Mashariki.“Watu wanaoaminika kuwa wa familia moja, walikuwa wakisafiri kwa gari la Toyota Noah kutoka Juba kuelekea Nimule gari hilo lilipogonga lori la kusafirisha mafuta katika makutano ya barabara ya Amee,” Msemaji wa Polisi alisema.

Jumatatu.

You can share this post!

Waathiriwa wa mlipuko wazikwa

#KUMEKUCHA: Shabiki wa Taifa Leo Mzee Paulo Mwanyalo...

T L