• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 12:09 PM
AFYA: Vidonda vya tumbo

AFYA: Vidonda vya tumbo

Na MARGARET MAINA

[email protected]

VIDONDA vya tumbo ni tatizo linalotokea baada ya kuta za tumbo au utumbo mdogo kuwa na vidonda.

Hali hii hutokea baada ya kuharibika kwa ukuta wenye ute unaozuia kemikali za kuyeyusha chakula.

Kemikali ambayo ni asidi inayozalishwa mwilini kiasili husaidia kuyeyusha chakula na kuua wadudu tumboni na kama ukuta wenye ute utaharibiwa na kushindwa kufanya kazi, basi hiyo kemikali (asidi) itaathiri tumbo au utumbo na kuruhusu bakteria kuendelea kusababisha vidonda vya tumbo.

Vidonda vya tumbo vinatibika kirahisi ila vikicheleweshwa bila kutibiwa huweza kusababisha tatizo kubwa.

Ni tatizo linalotesa sana na kuwanyima raha watu wengi. Pia husababisha magonjwa mengine kama kansa, amoeba (amiba), homa na kupungua uzani.

  • Vidonda vya tumbo kubwa (Gastric ulcers) – Hivi ni vidonda vya tumbo vinavyotokea ndani kwenye tumbo kubwa
  • Vidonda vya utumbo mdogo (Duodenal ulcers) – Hivi ni vidonda ambavyo hutokea kwenye utumbo mdogo (hasa juu)

Chanzo cha vidonda vya tumbo

Vidonda vya tumbo vina vyanzo tofauti ili vyote ni vile vinavyohusiana na mmeng’enyo. Vyanzo hivyo ni;

  • bakteria waitwao Helicobacter pylori (H. pylori)
  • matumizi ya dawa za kupunguza maumivu
  • kuwa na mawazo mengi
  • kula vyakula vinavyozalisha asidi kwa wingi
  • kunywa pombe na vinywaji vikali
  • uvutaji wa sigara
  • kukosa kula mlo kwa mpangilio

Dalili za vidonda vya tumbo

Dalili za vidonda vya tumbo hujitokeza baada ya kula au kabla ya kula, ila mara nyingi wengi huwa wanazipuuza na kuendelea kukuza tatizo. Vidonda vya tumbo vina dalili kama:

  • kupata maumivu ya tumbo yanayokuwa kama ya moto (kuunguza) baada na kabla ya kula
  • kusumbuliwa na kiungulia
  • tumbo kujaa gesi na kuvimbiwa
  • kichefuchefu na kutapika
  • kupoteza hamu ya kula na kupungua uzani
  • kushindwa kupumua vizuri

Cha kufanya ili kuepukana na vidonda vya tumbo

  • kunywa maji mengi
  • punguza mawazo, fanya mazoezi yatakuepushia mawazo
  • punguza kiwango cha halemu
  • usivute sigara
  • punguza au acha kunywa pombe
  • kula vizuri vyakula bora hasa asilia na sio vyakula vyenye kemikali
  • lala vizuri kwa muda mzuri, angalau saa 7 hadi 9

Maumivu yakizidi, pata ushauri wa daktari.

You can share this post!

Messi sasa mali rasmi ya PSG baada ya kutia saini mkataba...

Uhuru mbioni kufufua Nasa