NA FRIDAH OKACHI
ESTHER Musila, mke wa mwanamuziki wa nyimbo za Injili Guardian Angel, ametunukiwa cheti na shirika la Umoja wa Mataifa (UN) kwa kuwa miongoni mwa watu waliofanya kazi kwa kipindi kirefu kwenye shirika hilo.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Bi Musila alichapisha picha akiwa ameshikilia cheti ambacho ni tuzo kutoka kwa UN na kuandamanisha na ujumbe uliobainisha na kutambua kwamba amefanya kazi na UN kwa zaidi ya miaka 20.
“Imekuwa miaka 22 ya kutoa huduma kwa binadamu. Leo nimebahatika kuwa miongoni mwa wafanyikazi waliotunukiwa Tuzo ya Kutumikia Shirika kwa Muda Mrefu. Utukufu na heshima zote kwa Mungu,” alichapisha.
Bi Musila aliendelea kijapisha ujumbe mwingine akijishukuru binafsi kwa kufanya kazi kwenye shirika la UN na kuwa mwaminifu kwa kipindi chote. Ni kazi ambayo ameisifia akisema imeleta mabadiliko makubwa kwenye jamii.
“Miaka 22 na bado inahesabika. Ninataka kujishukuru kwa uaminifu wangu kwa Umoja wa Mataifa na kuamini kutoa michango yenye matokeo katika wajibu wangu wa huduma. Nashukuru Esther. Mungu amekuwa mwaminifu kweli,” alichapisha Musila.
Ni tuzo ambayo wanatunukiwa wafanyakazi wa UN ikiwa ni ishara ya kuleta amani na kujituma.
Bi Musila, 53, aliolewa na mwanamuziki Guardian Angel, 31.
Mnamo Januari 2023, mume wake alisherekea siku ya kuzaliwa ya Gilda ambaye ni mwanawe Bi Musila mwenye umri wa miaka 29 sasa, akimtakia maisha yenye baraka.
“Ubarikiwe kupita kipimo. Heri ya siku ya kuzaliwa G. @onlygilda . Nakupenda. Mungu akubariki kwa ajili yetu,” Guardian alichapisha kwa ukurasa wake wa Instagram.
Mwaka 2022, wawili hao walisutwa na mashabiki kwa kuishi pamoja, shabiki mmoja akitaka kufahamu ni lini wangepata mtoto.
Swali hilo lilimkera Bi Musila na kumjibu: “Hiyo inaongeza thamani ya maisha yako vipi?”