• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
UDAKU: Binti wa Guardiola abaki kwa mataa Dele Alli akirukia kipusa Nicole

UDAKU: Binti wa Guardiola abaki kwa mataa Dele Alli akirukia kipusa Nicole

Na CHRIS ADUNGO

KIUNGO mvamizi wa Tottenham Hotspur, Dele Alli, sasa ameanza kumtambalia kimapenzi mwanahabari maarufu wa Chelsea TV, Nicole Berry.

Alli amekuwa akitafuta mpenzi wa kudumu naye tangu kipusa Ruby Mae amteme rasmi miezi sita iliyopita.

Ruby, ambaye amewahi kuwa balozi wa mauzo wa bidhaa za Dolce & Gabbana pamoja na Chanel, alianza kutoka kimapenzi na Alli mnamo 2016.

Walitengana kwa mara ya kwanza mnamo 2018 kabla kurudiana.Kutemwa kwa Alli kulichangiwa na mazoea yake ya kutumia muda mwingi kushiriki michezo ya mitandaoni, huku akiacha demu wake akipigwa na baridi usiku kucha.

Mwanasoka huyo amekuwa akionekana mara kwa mara na Maria, ambaye ni binti wa kocha Pep Guardiola wa Manchester City.

Ni matukio yaliyoaminisha mashabiki kwamba wawili hao wamekuwa wakila bata.

Akihojiwa na gazeti la The Sun wiki iliyopita, Alli alishikilia kwamba kubwa zaidi katika mipango yake kwa sasa ni kutulia katika ndoa, na dalili zote zinaashiria kwamba Nicole ndiye atakayeishi naye raha mustarehe kwani anapanga kumvisha pete ya uchumba.

Hata hivyo, alikataa kuzungumzia uhusiano wake na Maria, ambaye alikuwa akiponda naye raha wiki tatu zilizopita katika hoteli moja jijini London, Uingereza.

Kabla ya hapo, Alli, 25, aliwahi pia kuonekana na Maria, 20, wakijistarehesha katika hoteli nyingine ya kifahari eneo la Mayfair, Uingereza.

Katika mojawapo ya picha zilizopakiwa na Alli mtandaoni wiki iliyopita, nyota huyo alionekana akikamata mkono wa Nicole huku kipusa huyo raia wa Canada akiegemeza kichwa chake kwenye bega la dume lake.

Kwa upande wake, Nicole, 24, alifichua kuwa Alli alianza kumtumia picha na video za mapenzi yapata miezi miwili iliyopita, baada ya kukutana naye kwenye programu ya Raya ya kutafuta wapenzi mitandaoni.

Kabla ya kuanza kumtambalia Maria, Alli alikuwa akichovya asali mzingani mwa mwigizaji maarufu Megan Barton-Hanson, anayemzidi umri kwa mwaka mmoja.

Alianza kuburudishwa na Megan, 26, mwezi mmoja baada ya kichuna huyo kutemana na Wes Nelson – mwigizaji mwenzake katika filamu za Love Island.

You can share this post!

Kibicho alalama kuhusu idadi ndogo ya watu waliojisajili

UDAKU: CR7 amfunga Georgina hat-trick safi ya mapenzi

T L