• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 12:36 PM
JAMVI: Kilio IEBC ikiendelea na chaguzi ndogo bila ya kampeni

JAMVI: Kilio IEBC ikiendelea na chaguzi ndogo bila ya kampeni

Na MWANGI MUIRURI

KANUNI zilizopitishwa hivi majuzi na serikali kuzuia ueneaji wa virusi vya corona, zimeanza kutoa taswira ya jinsi hali itakavyokuwa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022 endapo taifa litaendelea kulemewa na janga la corona.

Ijapokuwa kumekuwepo chaguzi ndogo nyingi tangu janga hilo lilipoingia nchini Machi mwaka uliopita, kampeni za hadharani kuhusu chaguzi zilizopangiwa kufanyika Mei 18, zimekwama.

Tume ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) inapania kuandaa chaguzi tatu ndogo katika mazingara mageni kabisa ambapo kampeni zimezimwa kufuatia masharti ya kupambana na janga la Covid-19.

Ingawa IEBC ilitoa mwanya wa kati ya Machi 29 hadi Mei 15 kwa wawaniaji kuvumisha kampeni zao, kwa sasa hali si hali kwa kuwa ubunifu ndio unahitajika ili kujipigia debe.

Chaguzi hizo zitaandaliwa katika maeneobunge ya Juja na Bonchari na katika wadi ya Rurii iliyoko kaunti ya Nyandarua. Uchaguzi mdogo wa Useneta Kaunti ya Garissa umefutiliwa mbali baada ya kuibuka mwaniaji mmoja tu ambaye ni Abdul Haji na ikabidi atawazwe mshindi wa kumrithi babake Yusuf Haji aliyeaga.

Tayari, baadhi ya wawaniaji wameanza kulia wakisema kwamba chaguzi hizo zinafaa ziahirishwe hadi wakati kutakuwa na mwanya wa kufanya kampeni za kukutanisha watu moja kwa moja wachumbiwe.

Hali haswa ni ngumu zaidi kwa wawaniaji 12 wa Juja—eneobunge ambalo liko katika Kaunti ya Kiambu—ambako hata baa na hoteli zimeagizwa kufungwa hivyo basi kuzima mianya yote ya kuwafikia wapigakura moja kwa moja.

Ni katika hali hiyo ambapo Bw Joseph Njoroge Mburu ametoa ilani ya hadi Jumanne wiki ijayo kwa IEBC akiitaka iahirishe chaguzi hizo hadi wakati hali ya kawaida itakaporejea.

La sivyo, amesema kuwa ataandaa kesi ya kuomba mahakama ishinikize IEBC kutangaza kuahirishwa kwa chaguzi hizo.

Bw Mburu ambaye anawania Juja kwa tiketi ya People Party of Kenya (PPK) analia kuwa “hatuwezi tukazimwa kufanya kampeni kisha tutarajiwe kushindana katika uwanja ulio na usawa na uwazi.

Baadhi ya wagombeaji wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii na SMS kuvumisha ajenda zao.

Hata hivyo, kuna changamoto kwa vile tofauti na mikutano ya hadhara, wameshindwa kujua jinsi jumbe hizo zinapokewa na wapigakura.

Akahoji: “Mpigakura ambaye hata kujinunulia barakoa ya Sh5 ni shida, aliye na mahangaiko ya kufungiwa riziki kufuatia matangazo hasi ya kupambana na Covid-19 ambayo hayaambatanishwi na mikakati ya kutoa afueni kwao, aliye na mahangaiko ya gharama kubwa ya maisha…utamwambia namna gani atenge bajeti ya kugharamia intaneti ndio afuatilie kampeni za uchaguzi mdogo? Hata hiyo, raha na saa za kuketi chini azame mitandaoni eti anafuatilia kampeni atatoa wapi?”

Bw Mburu alisema kuwa sheria za uchaguzi hutoa mwanya wa kampeni za moja kwa moja kati ya wawaniaji na wapigakura “lakini kwa sasa hata mkutano wa watu wawili kwa msingi wa kisiasa umezimwa.”

Alisema kuwa kuendelea mbele na kuandaa uchaguzi huo ni sawa na kuwavizia wawaniaji hasa wale ambao hawana rasilimali za kulipia matangazo ya runinga na redio.”

Alisema kuwa chaguzi hizo zikiandaliwa kama ilivyoratibiwa, kutakuwa na mwanya mkubwa wa kutotoa taswira kamili ya umaarufu wa wawaniaji na ufaafu wao.

Mbunge wa Mugirango Kusini Silvanus Osoro anasema kuwa “ni wakati mgumu wa kuchapa kampeni kwa kuwa ni lazima pia uzingatie usalama wa kiafya kwa wapigakura na ukionekana kama unakaidi masharti yaliyowekwa, unagongwa na propaganda na wapinzani kuwa wewe ni sawa na muuaji ambaye analenga kuwamaliza wapigakura kwa kuwaambukiza corona.

Bw Osoro ambaye anashirikisha kampeni za United Democrativc Alliance (UDA) katika uchaguzi huo aliambia Taifa Jumapili kuwa “kwa sasa tunatumia mabango, mitandao ya kijamii na matangazo kwa vyombo vya habari ambavyo vinatangaza kwa lugha za mashinani ya kwetu kuwafikia watu.”

You can share this post!

Uingereza yapongezwa kwa kuwa na msimamo chanya kuhusu...

Sakaja amshukuru Rais Kenyatta kwa kutoa Sh1 milioni kumfaa...