NA CHARLES WASONGA
RAIS William Ruto anatekeleza mikakati mahsusi inayolenga kufifisha uasi unaoendeshwa na muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya dhidi ya serikali yake.
Kilele cha uasi huo ni maandamano ya kesho Jumatatu jijini Nairobi.
Duru zinasema hatua ya Rais Ruto kuwatunuku nyadhifa kubwa serikalini mahasidi wa Bw Odinga haswa kutoka ngome yake ya Luo Nyanza, kukaribisha jumbe za viongozi kutoka maeneo mbali mbali nchini katika Ikulu ya Nairobi na kutumia mabalozi wa mataifa ya kigeni kumwekea Odinga presha aachane na maandamano, ni miongoni mwa mikakati hiyo.
Kwa mfano, wiki hii Rais Ruto aliwateua kama mawaziri wasaidizi (CASs) wanasiasa kadhaa kutoka eneo la Nyanza ambao wamemuasi Bw Odinga na kuamua kufanyakazi na serikali ya Kenya Kwanza.
Wao ni aliyekuwa gavana wa Nairobi Evan Kidero, aliyekuwa Seneta wa Kisumu Fred Outa na aliyekuwa Mbunge wa Rarieda Nicholas Gumbo.
Dkt Kidero aliwania ugavana wa Homa Bay lakini akabwagwa na gavana wa sasa Gladys Wanga huku Bw Gumbo akiwania ugavana Siaya na kushindwa James Orengo.
Wachanganuzi wa masuala ya siasa wanasema kwa kuteua watatu hao kuwa mawaziri wasaidizi, na baadhi ya wabunge wa zamani kutoka Nyanza kama wanachama wa bodi za mashirika ya serikali, Rais Ruto analenga kuondoa dhana kuwa serikali yake inashirikisha watu kutoka maeneo yaliyompigia kura pekee; Mlima Kenya na Bonde la Ufa.
“Rais amewateua watu kama Kidero, Outa na wengine haswa kutoka Luo Nyanza kwa lengo la kuondolea mbali malalamishi ya kila mara ya Bw Odinga kwamba teuzi zake ni za kikabila. Kumbuka kuwa hili ni mojawapo ya malalamishi 15 ambayo Raila na wenzake walitaja kwenye makataa yao kwa serikali kabla ya kuitisha maandamano,” anasema Dkt David Magut.
Hatua ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Noordin Haji kusitisha uchunguzi dhidi za Waziri wa zamani wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i pia inasawiriwa kama mkakati mwingine ambao Rais Ruto anatumia ili kudhoofisha umaarufu wa Bw Odinga katika eneo pana la Gusii.
“Bila shaka Rais Ruto ndiye aliamuru kwamba uchunguzi dhidi ya Dkt Matiang’i usitishwe. Hii ni baada ya suala hili kuchukua mkondo wa kisiasa wanasiasa na watu kutoka eneo la Gusii walipolifasiri kama dhuluma dhidi ya jamii hiyo,” anasema Bw Martin Andati ambaye ni mchanganuzi wa masuala ya kisiasa.
Seneta wa Kisii Richard Onyonka anasema Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) iliamriwa kusitisha uchunguzi dhidi ya Dkt Matiang’i, kuhusiana na madai kuwa polisi walivamia makazi yake, baada ya wao kama viongozi wa Gusii “kumwekea Rais Ruto presha za kisiasa”.
“Na Rais Ruto hakuwa na jingine ila kusalimu amri kwa sababu atataka kutetea kiti chake katika uchaguzi mkuu wa 2027,” akasema Jumanne asubuhi kwenye mahojiano katika runinga ya Citizen.
Bw Odinga pia amekuwa mstari wa mbele kupinga kile alichokitaja kama “kuhangaishwa kwa Dkt Matiang’i kutokana na sababu za kisasa.”
Mnamo Februari 8, kiongozi huyo wa Azimio alikuwa mstari wa kwanza kufika katika makazi ya Waziri huyo wa zamani mtaani Karen, Nairobi, mwendo wa saa nne za usiku, baada ya kupokea habari kwamba maafisa wa polisi walitaka kuyavamia.
Aidha, wiki jana, Bw Odinga alifika katika makao makuu ya DCI “kumtetea” Dkt Matiang’i ambaye alikuwa amefika huko kuandikisha taarifa kuhusu madai kuwa alitoa habari za uwongo kwamba polisi walipanga kuvamia makazi yake.
“Kwa ‘kumsamehe’ Dkt Matiang’i, Rais Ruto sasa amefaulu kuonyesha jamii ya Abagusi kwamba yeye ndiye mwenye uwezo na nguvu ya kuwasaidia bali sio Bw Odinga,” Bw Andati anaongeza.
Lakini Profesa Macharia Munene anasema presha kutoka kwa jamii ya kimataifa na maafisa wa kidiplomasia ndizo huenda Rais Ruto akategemea zaidi kumtuliza Bw Odinga.
“Bila shaka jamii ya kimataifa haiwezi kukaa kitako ikitizama Kenya ikiteketea ilivyofanyika baada ya uchaguzi mkuu wa 2007. Hii ni kwa sababu Kenya ni muhimu zaidi haswa katika kuyawezesha mataifa ya magharibi kama vile Uingereza na Amerika kuendeleza mipango yao katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. Mojawapo ya mipango hiyo ni vita dhidi ya ugaidi,” anasema Profesa Macharia ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Amerika (USIU), bewa la Kenya.
Duru zimeiambia meza ya Jamvi la Siasa kwamba mnamo Jumanne Bw Odinga mwenyewe alikiri mbele ya baadhi ya wabunge wa ODM kwamba amekuwa akipokea presha kutoka kwa baadhi wa mabalozi wa mataifa ya kigeni wakimtaka kusitisha maandamano ya kesho.
“Ni kweli kwamba Raila amewekewa presha nyingi na mataifa ya kigeni haswa yale ya magharibi. Alitueleza yale ambayo anapitia na tukashangaa zaidi,” anasema mbunge mmoja wa ODM aliyehudhuria mkutano wa wabunge kutoka Luo Nyanza uliofanyika katika makazi ya Mbunge wa Nyando Jared Okelo.
Bw Odinga alihudhuria mkutano huo ambao uliitishwa kujadiliwa mikakati ambayo wabunge wa eneo hilo watatumia kupambana na wanasiasa waasi kutoka eneo hilo ambao juzi walijiunga na chama cha United Democratic Alliance (UDA).
Aidha, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka amethibitisha kuwa Azimio inapokea presha kutoka kwa jamii ya kimataifa ikomeshe maandamano.
“Inasikitisha kuwa serikali ya Ruto inatumia mabalozi ya kigeni kutuwekea presha tusitishe mchakato huu wa kutetea haki ya Wakenya. Tunaonya jamii ya kimataifa dhidi ya kuingilia masuala ya ndani ya taifa huru kama Kenya. Watuache tusuluhishe changamoto zetu kivyetu,” Bw Kalonzo akasema Alhamisi katika mkutano wa Azimio jijini Nakuru.
Subscribe our newsletter to stay updated