• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:07 PM
KINYUA BIN KING’ORI: Ruto afikirie upya kuhusu kubuni miungano, hafai kuipuuza

KINYUA BIN KING’ORI: Ruto afikirie upya kuhusu kubuni miungano, hafai kuipuuza

Na KINYUA BIN KING’ORI

MALUMBANO na mgawanyiko ambao umeanza kujitokeza katika mrengo unaomuunga mkono Naibu Rais, Dkt William Ruto katika kuwania urais 2022 hayajengi bali kubomoa na kufifisha nyota ya kinara huyo wa kambi ya Hasla.

Wabunge wanaompigia debe Dkt Ruto husasan katika eneo la Mlima Kenya wameanza kuzozana na wenzao wanaotaka kuruhusiwa kutumia vyama vyao vya kisiasa kushirikiana na naibu huyo wa rais kubuni miungano ya kisiasa tukielekea uchaguzi mkuu ujao wa 2022.

Washirika damu wa Dkt Ruto katika Mlima Kenya kwenye kikao chao majuzi walisisitiza kuwa watatumia chama cha UDA kushinikiza maslahi yao kushirikishwa katika serikali ijayo.

Mtazamo huo unakinzana pakubwa na maoni ya aliyekuwa waziri wa Kilimo Mwangi Kiunjuri aliyefutwa kazi Kwa kuhusishwa na Naibu Rais ambaye kwa sasa amebuni chama cha TSP na kukaidi uamuzi wa kuvunjwa kwa vyama vingine ili watumie chama kimoja cha UDA.

Bw Kiunjuri ni mwanasiasa mpevu, mwenye tajriba kisiasa na mkakamavu katika usemi na maoni yake hayafai kupuuzwa.

Kubuni vyama kama vile TSP hakutaifaa jamii ya Mlima Kenya katika ulingo wa kisiasa katika kudai haki katika mgao wa rasilimali serikalini.

Kundi la Mbunge Rigathi Gachagua likome kuchukuliwa kama lenye misimamo tofauti kama maadui wao kisiasa.

Hakuna haja ya wafuasi hao wa Bw Ruto kulaumiana bure. Kutoa matamshi yenye kuchochea na kujenga uhasama katika kundi lao ilhali wote wanakubaliana kumuunga mkono Naibu Rais katika kuwania urais hakufai.

Itabidi Dkt Ruto mwenyewe kukubali mambo si shwari tena anavyohadaika atazoa kwa wingi kura za eneo la Kati 2022 liwe liwalo.

Anafaa kusuka mikakati upya na kuwa mnyenyekevu, mpole asiye na kiburi ili afaulu kuwaunganisha wafuasi wake Mlimani bila kujali vyama vyao kisiasa.

Naibu Rais ingawa kweli anao umaarufu kwa sasa kisiasa kutokana na jinsi anavyoendesha kampeni zake kujivumisha mashinani kwa mikakati kabambe, ikiwa kweli anataka kushinda urais lazima akubali kukumbatia vyama vingine vinavyomuunga mkono kushirikiana na UDA bila kulazimishwa kuvivunja.

Ili kupambana na Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga ambaye ni mwanasiasa jasiri na mjanja katika siasa za miungano, Dkt Ruto hana budi kulinda uhai wa kisiasa na umaarufu wake kwa kuhakikisha ameokoa dau lake lisizame kwa kuwaunganisha hata ikimaanisha kuwabembeleza.

Bila kuficha, ili kiongozi yeyote kufaulisha ndoto ya kuingia ikulu kwa namna yoyote ile lazima awe mwenye kusuka miungano ya kisiasa na zaidi ya chama kimoja na Dkt Ruto hafai kudharau hilo.

Na miungano hiyo inafaa kabla ya uchaguzi wa 2022.

Si hatia nchini wanasiasa kubuni miungano kwa manufaa ya watu wao kisiasa, hivyo UDA ikome kiburi ikiwa kweli inataka kiongozi wake apate uungwaji mkono wa kujivunia kote nchini.

Waige Bw Raila ambaye yu mbioni kuunda miungano ya kisiasa na wanasiasa wa vyama vingine kwa azma ya kuimarisha nafasi ya kumrithi Rais Uhuru Kenyatta akistaafu.

Dkt Ruto anapaswa kufanya maamuzi mapema kuepuka kupoteza wanasiasa waliokuwa wameanza kumuunga mkono katika azma yake kugombea urais kwa kufanya mashauriano na vyama vingine.

You can share this post!

Maelfu bado wapigania kuenda Saudia

Hawana jipya hao, Mutua awasuta viongozi wa OKA