NA SAMMY WAWERU
WANAMAZINGIRA na wanasheria nchini wamezindua kitabu chenye kuchunguza na kuainisha utekelezaji wa mfumo wa sheria za mazingira Kenya kama kama ulivyotajwa kwenye Katiba.
Kitabu hicho, “Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba,” kinajadili kuhusu uhifadhi wa mazingira na kutoa maudhui yenye mafunzo kwa wanafunzi, watafiti, na maafisa wa serikali wanaojihusisha na sera za umma.
Shabaha ya kitabu hicho vilevile ni kuelewa kuhusu mada muhimu kama vile hali ya hewa, uchafuzi wa mazingira, usimamizi wa maji, mimea na mazao ya GMO, bioteknolojia, na mapendekezo kutatua migogoro katika maeneo kame na nusu-kame (ASAL).
“Migogoro inayojitokeza mara kwa mara nchini kama vile vita vya kijamii kuhusu mifugo na malisho, imetokana na athari za mabadilio ya tabianchi. Ni muhimu tuanze kuitatua kwa kuangazia mazingira,” alisisitiza Dkt Robert Kibugi, Mhadhiri Mkuu katika Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu cha Nairobi (UoN).
Alisema hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa kitabu hicho katika makao makuu ya chuo hicho jijini Nairobi.
Aidha, Dkt Kibugi ni mmoja wa wahariri watatu wa kitabu hicho.
Uzinduzi wa kitabu hicho unajiri wakati ambapo viongozi wa mataifa mbalimbali ulimwenguni wanaendeleza mjadala jinsi ya kuangazia athari chanya za mabadiliko ya tabianchi yanayojumuisha masuala kama ongezeko la kiwango cha joto duniani na ukame.
Aidha, mabadiliko ya hali ya hewa yamesababisha mchipuko wa wadudu waharibifu na magonjwa.
Prof Patricia Kameri-Mbote, Mkurugenzi Idara ya Sheria katika Mpango wa Mazingira ya Umoja wa Mataifa (UNEP) na mwandishi mkuu wa kitabu hicho, alisisitiza umuhimu wa kujenga njia ya utangamano kati ya Wanasayansi na wataalamu wa sheria.
Kulingana na Prof Patricia, ushirikiano huu utaunda mazingira yanayowezesha kushughulikia changamoto za hali ya hewa zinazokabili dunia.
Uzinduzi wa kitabu hicho umejiri miezi michache kabla ya Kongamano la Umoja wa Mataifa Kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi, Makala ya 28, ndio, United Nations Climate Change Conference au Conference of the Parties of the UNFCCC (COP28) kufanyika.
Kongamano la mwaka huu limeratibiwa kufanyika Dubai kati ya Novemba 30 hadi Desemba 12.
Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba, ni Kitabu chenye sura 27 na kimeandikwa na waandishi 36 kutoka utandawazi wa mazingira na sheria.
Nakala ya kidijitali itapatikana bila malipo yoyote, kupitia tovuti ya UNEP.