• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:50 AM
Kitabu kuelimisha sheria za mazingira na kuyahifadhi  

Kitabu kuelimisha sheria za mazingira na kuyahifadhi  

NA SAMMY WAWERU

WANAMAZINGIRA na wanasheria nchini wamezindua kitabu chenye kuchunguza na kuainisha utekelezaji wa mfumo wa sheria za mazingira Kenya kama kama ulivyotajwa kwenye Katiba.

Kitabu hicho, “Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba,” kinajadili kuhusu uhifadhi wa mazingira na kutoa maudhui yenye mafunzo kwa wanafunzi, watafiti, na maafisa wa serikali wanaojihusisha na sera za umma.

Bw Agostinho Neto (kulia), ambaye ni afisa wa serikali akizindua nakala ya kitabu cha “Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba” katika Chuo Kikuu cha Nairobi. PICHA|SAMMY WAWERU

Shabaha ya kitabu hicho vilevile ni kuelewa kuhusu mada muhimu kama vile hali ya hewa, uchafuzi wa mazingira, usimamizi wa maji, mimea na mazao ya GMO, bioteknolojia, na mapendekezo kutatua migogoro katika maeneo kame na nusu-kame (ASAL).

“Migogoro inayojitokeza mara kwa mara nchini kama vile vita vya kijamii kuhusu mifugo na malisho, imetokana na athari za mabadilio ya tabianchi. Ni muhimu tuanze kuitatua kwa kuangazia mazingira,” alisisitiza Dkt Robert Kibugi, Mhadhiri Mkuu katika Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu cha Nairobi (UoN).

Profesa Patricia Kameri-Mbote, Mkurugenzi Idara ya Sheria katika UNEP akijadiliana na mtaalamu wa mazingira kuhusu nakala ya kitabu cha “Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba” kilichozinduliwa katika Chuo Kikuu cha Nairobi. PICHA|SAMMY WAWERU

Alisema hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa kitabu hicho katika makao makuu ya chuo hicho jijini Nairobi.

Aidha, Dkt Kibugi ni mmoja wa wahariri watatu wa kitabu hicho.

Profesa Patricia Kameri-Mbote, Mkurugenzi Idara ya Sheria katika UNEP akitia saini nakala ya kitabu cha “Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba” kilichozinduliwa katika Chuo Kikuu cha Nairobi. PICHA|SAMMY WAWERU

Uzinduzi wa kitabu hicho unajiri wakati ambapo viongozi wa mataifa mbalimbali ulimwenguni wanaendeleza mjadala jinsi ya kuangazia athari chanya za mabadiliko ya tabianchi yanayojumuisha masuala kama ongezeko la kiwango cha joto duniani na ukame.

Aidha, mabadiliko ya hali ya hewa yamesababisha mchipuko wa wadudu waharibifu na magonjwa.

Kutoka Kushoto, Agostinho Neto, Profesa Patricia Kameri-Mbote, Mkurugenzi Idara ya Sheria katika UNEP, na Michael Onyango, Naibu Mkurugenzi Mkuu Mtendaji Alliance for Science, wakikagua nakala ya kitabu cha “Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba” kilichozinduliwa katika Chuo Kikuu cha Nairobi. PICHA|SAMMY WAWERU

Prof Patricia Kameri-Mbote, Mkurugenzi Idara ya Sheria katika Mpango wa Mazingira ya Umoja wa Mataifa (UNEP) na mwandishi mkuu wa kitabu hicho, alisisitiza umuhimu wa kujenga njia ya utangamano kati ya Wanasayansi na wataalamu wa sheria.

Kulingana na Prof Patricia, ushirikiano huu utaunda mazingira yanayowezesha kushughulikia changamoto za hali ya hewa zinazokabili dunia.

Wataalamu wa mazingira, Wanasayansi na wanasheria wakionyesha kitabu cha “Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba” kilichozinduliwa katika Chuo Kikuu cha Nairobi. PICHA|SAMMY WAWERU

Uzinduzi wa kitabu hicho umejiri miezi michache kabla ya Kongamano la Umoja wa Mataifa Kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi, Makala ya 28, ndio, United Nations Climate Change Conference au Conference of the Parties of the UNFCCC (COP28) kufanyika.

Kongamano la mwaka huu limeratibiwa kufanyika Dubai kati ya Novemba 30 hadi Desemba 12.

Agostinho Neto (kulia) akimkabidhi Michael Onyango, Naibu Mkurugenzi Mkuu Mtendaji Alliance for Science kitabu cha “Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba” kilichozinduliwa katika Chuo Kikuu cha Nairobi. PICHA|SAMMY WAWERU

Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba, ni Kitabu chenye sura 27 na kimeandikwa na waandishi 36 kutoka utandawazi wa mazingira na sheria.

Nakala ya kidijitali itapatikana bila malipo yoyote, kupitia tovuti ya UNEP.


Bw Agostinho Neto (kulia), ambaye ni afisa wa serikali akijadiliana na baadhi ya wataalamu wa mazingira na Wanasayansi kuhusu nakala ya kitabu cha “Utawala wa Mazingira Nchini Kenya: Utekelezaji wa Mfumo wa Kikatiba” katika Chuo Kikuu cha Nairobi. PICHA|SAMMY WAWERU
  • Tags

You can share this post!

Haiti: Kenya ikae chonjo isiingie mtego wa Amerika

Tunaomba uvumilivu kidogo tu tunatengeneza uchumi, Weta na...

T L