NA SAMMY WAWERU
MBUNGE wa Kinangop Kwenya Thuku ametaja ufugaji ng’ombe wa maziwa Nyandarua kama mojawapo ya biashara zenye mapato ya kuridhisha, kufuatia kuimarika kwa bei ya maziwa.
Hata ingawa kauli ya mbunge huyo haiwiani na taswira nyanjani, alisema wafugaji Nyandarua wanavuna hela kupitia uuzaji maziwa kufuatia mikakati ya serikali kukuza sekta ya ufugaji.
“Mfano, kwetu Kinangop ufugaji ng’ombe wa maziwa umenoga kwa sababu ya bei bora ya maziwa,” Bw Kwenya alisema.
Alisema maendeleo hayo yanatokana na sera za Rais William Ruto kuboresha sekta ya kilimo na ufugaji nchini.
Biashara ya maziwa imeimarika kiasi wakulima wanatafuta ng’ombe kwa udi na uvumba, Kwenya alisisitiza.
“Kwa sasa, lita moja inachezea kati ya Sh45 – 50 jambo ambalo halijawahi kushuhidiwa Nyandarua,” alielezea.
Mbunge huyo alitoa kauli hiyo katika ziara ya Rais Ruto Kinangop majuzi, ambapo kiongozi wa nchi alizindua miradi ya ujenzi wa barabara eneo hilo.
Kwa muda mrefu, ufugaji wa ng’ombe wa maziwa nchini umekuwa ukipitia changamoto tele kutokana na bei mbovu ya maziwa.
Mfano, Nyandarua visa vya wafugaji kumwaga maziwa kwa sababu ya soko duni vimekuwa vikiripotiwa.
Isitoshe, gharama ya malisho inazidi kulemea wakulima.