• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 5:20 PM
NDIVYO SIVYO: Neno ‘mgombea-mwenza’ na mitego yake kimatumizi

NDIVYO SIVYO: Neno ‘mgombea-mwenza’ na mitego yake kimatumizi

MIKTADHA tofauti ya matumizi ya dhana ‘mgombea mwenza’ inadhihirisha kuwepo kwa mgongano wa kimaana baina ya dhana yenyewe na aina nyingine za maneno, kwa mfano, vivumishi.

Kosa jingine linatokana na matumizi ya ‘mgombea’ katika hali ya wingi pamoja na ‘mwenza’ katika hali ya umoja hivyo basi kuibuka na dhana ‘wagombea mwenza’.

Kosa hili linajitokeza katika maelezo yafuatayo: ‘‘…*washirika wengine wa Dkt Ruto kutoka eneo la Mlima Kenya waliopigiwa upatu kuwa wagombea mwenza wake…’’

Nomino mgombea inatokana na kitenzi gombea ambacho kina maana tatu. Kwanza ni kushindania kitu. Pili, ni kuingia katika mashindano ya uchaguzi huku ukipania kuchaguliwa. Tatu, ni kuwa upande mmoja katika pande mbili zinazoshindania kitu. Maana ya tatu yamkini ndiyo iliyoshirikishwa katika kuunda dhana tunayoirejelea.

Katika baadhi ya kamusi, mwenza na mwenzake ni vidahizo viwili. Hata hivyo, kwa maoni yangu, neno la kwanza ni ufipisho wa lile la pili.

Kwa hivyo, fasili ya maneno yenyewe inapaswa kuwa moja na inayorejelea mtu anayefanya kazi au shughuli fulani na mwingine au rafiki yake.

Nomino ‘mgombea’ na ‘mwenza’ zinapotumiwa pamoja, ‘mwenza’ hutekeleza dhima ya kivumishi cha jina. Hata hivyo, ndani ya kivumishi hiki inajitokeza dhana nyingine ya umilikishi. Umilikishi huo pia huwakilishwa na kivumishi cha A-unganifu {wa} na kile cha umilikishi ‘wake’ ambavyo vinapotumiwa pamoja na dhana ‘mgombea mwenza’ husababisha kosa la kujirudia inavyojitokeza katika maelezo: *‘…Naibu Rais William Ruto alidai kuwa mchakato wa mgombea mwenza wake ulichukua saa 17…’’

YATAENDELEA

You can share this post!

KAULI YA WALLAH BIN WALLAH: Kamwe huwezi kufanikiwa...

Malumbano ya Sonko, Haji yazidi kutokota

T L