• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
PAUKWA: Ujanja wanusuru Msanii asifutwe kazi na Kaburu

PAUKWA: Ujanja wanusuru Msanii asifutwe kazi na Kaburu

NA ENOCK NYARIKI

JIONI watalii na waelekezi wao walirejea vilipokuwa vyumba vya kupanga.

Juma, mkuu wa Idara ya Parachuti, aliondoka moja kwa moja kuenda kumwona Bwana Kaburu.

Ofisi ya Bwana Kaburu ilikuwa katika Idara ya Upangaji zilipokuwa pia ofisi nyingi za wakuu wa idara mbalimbali mbugani.

Juma, alizungusha kitasa cha mlango wa ofisi ya bosi wake akaingia.

Mwanamume mfupi mnene mwenye kitambi kilichoshuka na pua ndefu mfano wa kitara alikuwa ameketi kwenye kiti cha kubembea nyuma ya meza pana.

Macho ya Bwana Kaburu yaliwaka kama cheche za moto na midomo kumchezacheza. Alimtazama mfanyakazi wake kwenye kipaji cha uso kana kwamba jibu alilolitaka lilijisawiri huko.

Moyo wa Juma ulimdekadeka kwa wasiwasi asijue hatia yake.

“Ninataka urudi katika Idara ya Parachuti umlete mwenzako ambaye ni kiguru,’’ Bwana Kaburu alimwambia Juma.

Juma alisimama kwenye ofisi ya mkuu wake kwa takriban dakika tano akijaribu kupiga darubini kuhusu mtu aliyetumwa kumwita. Idara ambayo alikuwa ameteuliwa kuiongoza haikuwa na mwanamume mwenye sifa alizotajiwa na Bwana Kaburu.

“Bosi, mtu kama huyo hayuko idarani,’’ Juma alisema kwa unyenyekevu.

“Kwa nini mimi mwenyewe nilimwona mtu huyo – tena mwenye midomo iliyopinda – akidoea mabaki yaliyoachwa na wageni?” Bwana Kaburu alisema kisha akaendelea, ‘‘nimesema uje naye mara moja!’’

Juma hakutaka kuendelea kubishana na bosi wake. Alienda idarani kumtafuta mtu ambaye bosi wake aliisawiri picha yake. Msako wake haukuzaa matunda si jioni hiyo tu bali siku iliyofuata!

  • Tags

You can share this post!

Raila: DCI haiwezi kufanya uchunguzi huru kwa sababu Amin...

TAHARIRI: Kuongeza ada ya maji kutakwamisha maendeleo

T L