Na MWANDISHI WETU
RAIS wa Uganda Yoweri Museveni alieleza hali yake ya kiafya baada ya kuugua ugonjwa wa Covid-19.
Kwenye ujumbe wake mtandaoni, Rais Museveni alisema kuwa Ijumaa, Juni 9, 2023 ilikuwa siku yake ya tatu baada ya kupata ugonjwa huo.
Akisimulia jinsi alivyokuwa akihisi Jumatano a Alhamisi, rais huyo aliwaomba wananchi wake kupewa chanjo dhidi ya ugonjwa huo.
“Jana, Alhamisi (Juni 8, 2023) saa tano hivi asubuhi nilianza kuhisi usingizi mwingi licha ya kulala vizuri usiku uliotangulia. Hata hivyo, nilala mpaka saa tisa mchana. Nilipoamka, nilijihisi vyema na nikaandika hotuba ndogo itakayowasilishwa na Waziri Mkuu Nabbanja huko Luwero. Nilimtuma Nabbanja kwa sababu Makamu wa Rais Alupo anawakilisha nchi katika mkutano wa COMESA, Lusaka Zambia,” akaandika.
Aliongeza, “Nililala tena saa nne usiku na niliamka saa tisa usiku nikihisi maumivu kichwani. Niliketi na kunywa maji kama nilivyoshauriwa na binti yangu Patience na maumivu yakaisha.”
Rais Museveni alieleza kuwa kulingana na daktari wake wa muda mrefu Diana Atwiine, ugonjwa huo unaweza ukadhibitiwa kwa kula matunda na vyakula vyenye Vitamini C na D na dawa zilizo na histamini.
“Wakati Atwiine alitangaza hali yangu ya afya, nilimshauri kufanya hivyo kwa sababu nilikuwa nimeshikana na mambo mengine,” akaeleza.
“Nitasubiri siku zingine mbili kisha nipimwe tena. Inaonekana kupewa chanjo na kumeza dawa kunasaidia. Nitawaarifu.”