• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 10:50 AM
TAHARIRI: Serikali iwakinge wananchi maskini

TAHARIRI: Serikali iwakinge wananchi maskini

KITENGO CHA UHARIRI

BAADA ya vilio vya muda mrefu kuhusu gharama kubwa ya mafuta na maisha kwa jumla, hatimaye serikali inaonyesha dalili za kuwapunguzia raia wake, hasa maskini mzigo huo.

Juma lijalo bunge litajadili kuhusu viwango vya ushuru kwa dhamira ya kuvirejesha chini kwa angaa nusu

Kwa sasa ushuru wa VAT pekee kwa mafuta na gesi ni asilimia 16 na ndiyo sababu ya kupaa kwa bei za bidhaa hizo muhimu ambazo miaka kadhaa iliyopita ushuru wake ulikuwa chini mno.

Nyongeza ya bei za mafuta na gesi, iliyotokana na ushuru huo wa asilimia 16, inatishia kuwasukuma raia katika umaskini zaidi hasa inapozingatiwa kuwa tayari wamefinywa na makali ya janga la corona.

Kwa sasa, mtungi mdogo wa gesi (kilo 6) uliokuwa ukiuzwa karibu Sh1,000 hadi kufikia Mei mwaka huu sasa unauzwa kwa Sh1,400 huku mkubwa (kilo 13), uliokuwa ukiuzwa Sh2,100, sasa ukifika kati ya Sh2,500 na Sh2,900.

Mbali na VAT, kwa bidhaa za kimsingi, iliyokuwa imeongezwa kuanzia Julai 1, kupaa kwa bei za bidhaa hizo hasa mwezi huu kunatokana na hatua ya serikali ya kubuni ushuru wa ziada kwa bidhaa za kimsingi ikiwemo maziwa, sukari, mkate na nyinginezo mnamo Oktoba 1.

Japo bei ya mtungi wa gesi ilikuwa tayari imepanda kabla ya Oktoba 1, kuanzia juma hili, bei hiyo imeongezeka tena kwa angaa Sh200 kwa mtungimdogo na Sh400 kwa mtungi mkubwa.

Naam wapo watakaosema kuwa gesi ni ya watu wanaojiweza, lakini ukweli ni la; hilo si kweli.

Gesi siku hizi inatumika na watu wa matabaka yote hata mashambani ambako kawi iliyozoeleka kwa mapishi ni kuni.

Hiyo ina maana kuwa kuongezeka kwa bei ya bidhaa hizo kutaathiri vibaya hata watu wa tabaka la chini.

Kadhalika, kuongezeka kwa bei ya mafuta kunaathiri Wakenya wote maadamu shughuli nyingi za kiuchumi kwa sasa zinaendeshwa na mafuta; viwanda, magari ya uchukuzi na kadhalika.

Shughuli hizo humhusu kila Mkenya.

Kwa hayo yote, ushauri wetu ni kuwa bunge linapoketi juma lijalo kujadili bei za mafuta, vivyo hivyo, pawepo mjadala wa kupunguza bei za bidhaa nyingine muhimu hivi karibuni kabla ya madhara kuanza kushuhudiwa kote nchini.

Ni heri serikali ikose kiasi fulani cha ushuru lakini mwananchi aweze kuishi kwa kumudu riziki.

You can share this post!

Fatma ataka klabu za akina dada zijiunge kushiriki ligi ya...

AKILIMALI: Ni fundi stadi pale kwa mjengo; kubeba mawe,...