NA SAMMY WAWERU
KENCHIC ni mojawapo ya kampuni kubwa katika uzalishaji wa kuku nchini na ina mipango miwili kuhakikisha wateja wake wanapata mazao yaliyoafikia ubora: Farm to Farm, inalenga kusambazia wafugaji vifaranga walioanguliwa na kulelewa katika mazingira yaliyoafikia matakwa na vigezo vya kitaifa na kimataifa kuhusu wanyama na ndege.
Farm to folk, ni mpango wa ufugaji kuku, kuwachinja na kusambazia walaji nyama, na pia bidhaa zitokanazo na nyama za kuku hasa zilizoongezwa thamani.
Prisca Njeri, mfugaji wa kuku wa mayai Kiambu ni mmoja wa wafugaji wanaonufaikia kupitia mpango wa Farm to Farm, Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, Jim Tozer akisisitizia haja ya kuzalisha chakula salama kwa afya ya binadamu.
Njeri hununua vifaranga wake kutoka kampuni hiyo.
“Kinachotufikia mezani, sisi kama wadauhusika na washirika lazima tujitolee kuhakikisha ni salama. Mazao ya kuku ni kati ya yenye walaji wengi,” Tozer asema.
Aidha, Kenchic imeweka sheria na kanuni kali kuingia kwenye mazingira na vizimba vyake, ikiwemo kuoga na kubadilisha mavazi na viatu ili kuzuia msambao wa maradhi.
Isitoshe, imekumbatia mfumo huru kuendeleza ufugaji ambapo kuku hucheza na kuzurura kuonyesha maumbilehai yao.
Dkt Apollo Gichane, mtaalamu, anasema msimamo wa kampuni hiyo umesaidia kwa kiasi kikubwa kupata mazao salama.
“Gharama ya matibabu inakuwa ya chini,” adokeza, akishauri wakulima kuwa makini wanakotoa vifaranga.
Aidha, wanapaswa kuwa wamepata chanjo dhidi ya maradhi hatari kwa ndege.
Subscribe our newsletter to stay updated