• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
UDAKU: Drinkwater akaukiwa baada ya kutemwa

UDAKU: Drinkwater akaukiwa baada ya kutemwa

Na CHRIS ADUNGO

KICHUNA Carol Tozaki amemtema rasmi mwanasoka Danny Drinkwater ambaye ni raia wa Uingereza ili kujishughulisha zaidi na masuala ya uanamitindo nchini Brazil.

Uhusiano kati ya wawili hao unakatika baada ya kuwa pamoja kwa kipindi cha mwaka mmoja na nusu.

“Imebidi nitengane na Drinkwater ili nipate muda wa kutosha kuizamia taaluma yangu. Haikuwa vigumu kufikia maamuzi hayo kwa sababu naelewa ninachotaka kwa sasa,” akatanguliza.

“Iwapo Drinkwater ananipenda kwa dhati ya moyo na nafsi yake, basi atanisubiri nikamilishe ninachofanya kitaaluma ndipo tuoane baadaye,” akasema Carol wakati akihojiwa na gazeti la Jam Press nchini Brazil.

Drinkwater, 31, sasa anachezea kikosi cha Kasimpasa nchini Uturuki kwa mkopo kutoka Chelsea waliomsajili kutoka Leicester City mnamo 2017.

Mwishoni mwa Machi mwaka huu, Carol aliibuka mshindi wa taji la Miss Sao Paulo Intercontinental, mojawapo ya mapambano makubwa zaidi ya uanamitindo nchini Brazil.

Kipusa huyo anayejivunia zaidi ya mashabiki 47,000 kwenye Instagram amewahi pia kupamba ukurasa wa mbele wa jarida la masuala ya mapenzi la ‘No More’ nchini Brazil.

Drinkwater ambaye pia amewahi kuchezea Burnley na Aston Villa kwa mkopo kutoka Chelsea, aliwahi kupokezwa kichapo cha mbwa msikitini mnamo Septemba 2019 kwa jaribio kumtambalia kimapenzi mchumba wa mwanasoka mwenzake.

Kiungo huyo aliyekuwa amelewa chakari katika baa ya Chinawhite jijini Manchester, Uingereza, alianza kumnyemelea mchumba wa mwanasoka Kgosi Ntlhe wa kikosi cha Scunthorpe United, Uingereza.

Baada ya kukataliwa na demu aliyemsisitizia kwamba alikuwa na mpenziwe wakati huo, Drinkwater alizua kizaazaa na purukushani ndani ya baa huku akijigamba kuhusu jinsi anavyolipwa mshahara mnono wa hadi Sh13 milioni kwa wiki.

Maji yalipozidi unga, mabaunsa sita wa kilabu hicho cha Chinawhite walimfurusha Drinkwater nje na “kumfuza adabu.”

“Walimrukia na kumvaa mzima mzima. Walimkunja na kumkanyaga vibaya wakitaka kumvunja miguu. Walifahamu kwamba ni mwanasoka wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL). Walimuumiza vibaya na damu ilitapakaa kila mahali,” akasema mdokezi aliyeshuhudia kisa hicho wakati akihojiwa na gazeti la The Sun.

Kichapo hicho kutoka kwa mabaunsa kilimsaza Drinkwater na uso uliovimba, jicho lililoumia, mikono na mabega yaliyochubuka, shavu lililokatika na majeraha mabaya ya miguu. Alisalia mkekani kwa zaidi ya miezi miwili.

Kabla ya kujinasia penzi la Carol, Drinkwater alikuwa akiburudishwa na mwigizaji, mwanamitindo na mwanahabari shupavu mzawa wa jiji la Manhattan, Georgina Leigh Cantwell, 31.

Georgina ambaye pia anajulikana pakubwa kutumia urembo wake kuwatia kishawishi wanasoka wenye hela nyingi ndani na nje ya bara Ulaya, aliingia katika uhusiano wa kimapenzi na Drinkwater miezi saba baada ya kutemana na aliyekuwa mwigizaji mwenzake katika shoo ya Big Brother, Jackson Blyton.

You can share this post!

UDAKU: Alli aweka tangazo kwenye apu kusaka sogora wa...

MBWEMBWE: Fernandinho na mkewe ni wapenzi wa michuma ya bei...