KWA HISANI YA KENYA YEARBOOK
MOHAMMED Yusuf Haji alikuwa mmoja wa wakuu wa mikoa chini ya utawala wa chama cha KANU hadi 1997, alipoteuliwa Bungeni na Rais Daniel arap Moi.
Alibadilika umri ulivyozidi, akawa tofauti na awali- kwa mfano, mnamo Juni 1988, alikashifiwa kimataifa na mashirika ya kutetea haki za binadamu akiwa mkuu wa mkoa alipofanya mwanamume kufungwa jela kwa kukataa kumpa lifti.
Gari rasmi la kazi la Haji liliharibika na akasimamisha Peter Makau, mtaalamu wa stima aliyemjibu,
“Nenda ukatafute Gari la Serikali ya Kenya. Gari langu sio la serikali”.
Ndani ya saa chache, PC Haji alikuwa ameripoti suala hilo kwa Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Eldoret na mwanamume huyo akatiwa mbaroni.
Alifungwa jela kwa miezi mitatu siku iliyofuata na hakimu aliyesema “alikosa nidhamu… maafisa wa serikali wanapaswa kuheshimiwa. Mshtakiwa alikosa heshima na adhabu kali inapaswa kutolewa ili kuwa funzo kwa wale walio na akili na tabia kama yake.”
Haji aliyejiunga na utawala wa mikoa mwaka wa 1960 alihudumu kama afisa tawala, mbunge na kisha waziri wa ulinzi katika serikali ya Rais Mwai Kibaki.
Aliteuliwa waziri 2008 kufuatia Uchaguzi Mkuu wa 2007 aliochaguliwa mbunge wa Ijara kwa tikiti ya chama cha KANU.
Wakati huo, KANU kilikuwa kimojawapo cha vyama vilivyounga azma ya urais ya Kibaki kwa tikiti ya cha chama cha Party of National Unity (PNU).
Lakini uchaguzi huo ulikumbwa na ghasia baada ya chama cha Orange Democratic Movement (ODM) kikiongozwa na Raila Odinga kukataa matokeo na ghasia zikazuka Nairobi, sehemu za Rift Valley na Nyanza.
Ghasia hizo zilisababisha vifo vya watu 1400 na wengine 500,000 kufurushwa makwao na kufanya jamii ya kimataifa kuingilia kati kupatanisha Kibaki na Odinga.
Haji aliyezaliwa Desemba 23, 1940, alijulikana kwa utendakazi wake akiwa afisa wa utawala ambaye alihudumu sehemu tofauti za nchi chini ya serikali za Jomo Kenyatta, Moi, Kibaki na Uhuru Kenyatta na baadaye akiwa mwanasiasa chini ya Kibaki na Uhuru.
Kinyume na maafisa wengine wa utawala ambao walikuwa na elimu ya chuo kikuu, Haji alikuwa na cheti cha shule ya sekondari pekee kabla ya kujiunga na serikali na akafanya mtihani wa Maafisa wa Utawala katika Taasisi ya Utawala ya Kenya mwaka wa 1970.
Alilazimika kurudia tano kati ya kozi sita kisha akateuliwa mkuu wa wilaya mwaka wa 1981 na kupanda cheo hadi kuwa mkuu wa mkoa.
Mnamo Machi 2002, Moi alipokuwa akijiandaa kuondoka mamlakani, Haji alichaguliwa Mweka Hazina wa KANU na kudhihirisha kuwa mmoja wa watu waaminifu zaidi kwa Moi.
Vigogo wenzake katika chama hicho walipohama akiwemo George Saitoti, Kalonzo Musyoka, Joseph Kamotho na Moody Awori – wakilalamikia chaguo la Moi la Uhuru kuwa mrithi wake, Haji hakubanduka na akaamua kugombea kiti cha ubunge cha Ijara kwa tiketi ya KANU.
Wakati mkubwa wake William ole Ntimama, alijiuzulu kama Waziri katika Afisi ya Rais, Moi alimteua Haji, ambaye wakati huo alikuwa waziri msaidizi wa Ntimama kuchukua nafasi yake.
Katika serikali ya Muungano wa Kitaifa ambayo Kibaki alikuwa Rais na Odinga waziri mkuu baada ya ghasia za 2008, Haji aliteuliwa waziri wa Ulinzi.
Baadhi ya wasomi wanasema ni Haji aliyependekeza jeshi la Kenya kuingia Somalia na alitekeleza jukumu muhimu kuleta uthabiti katika nchi hiyo iliyokumbwa na vita.
Alitekeleza wajibu muhimu kupatanisha Ogaden National Front na serikali ya Ethiopia akiwa mwenyekiti wa kamati ya upatanishi kati ya 2012 na 2018.
Haji alishinda kiti cha useneta kaunti ya Garissa mwaka wa 2013 kwa tiketi ya Jubilee na kuchaguliwa mwanachama wa kamati ya seneti kuhusu ulinzi na Usalama wa Taifa.
Subscribe our newsletter to stay updated