• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 6:50 AM
WALIOBOBEA: Noah Wekesa ni daktari aliyejaribu siasa akavuna

WALIOBOBEA: Noah Wekesa ni daktari aliyejaribu siasa akavuna

KWA HISANI YA KENYA YEAR BOOK

NOAH Mahalang’ang’a Wekesa alikutana na Mwai Kibaki katika Chuo Kikuu cha Makerere.

Katika chuo hicho, Kibaki alikuwa ameibuka kuwa bingwa kwa werevu wake katika masomo.

Baada ya Makerere kushirikiana na Chuo Kikuu cha London kuwa Chuo Kikuu kamili mwaka wa 1949, Kibaki alikuwa mtu wa kwanza kuhitimu na Digrii ya Sanaa( kiwango cha juu zaidi) ya Chuo Kikuu cha London na kuweka historia katika chuo hicho mwaka wa 1955.

Kwa kijana Wekesa, ulikuwa mshangao asioweza kuuwazia. Wekesa alizaliwa Agosti 21 1936 katika kijiji cha Landweti, Kaunti ya Kakamega akiwa mwana wa Zacharia Mahalang’ang’a na Robai Khakasa.

Anatoka jamii ndogo wa jamii ya Waluhya ya Tachoni. Alianza masomo katika shule ya msingi ya Lokhokho mwaka wa 1945, kabla ya kuhamishiwa shule ya msingi ya Chevaywua umbali wa kilomita 16 kwenda na kurudi ambao alitembea kwa miguu.

Baadaye alihahamia shule ya msingi ya Lugulu Intermediate alipofanyia mtihani wa Kenya Primary Education mwaka wa 1951.

Wekesa alijiunga na shule ya sekondari ya Kaimosi na kisha shule ya upili ya Kakamega aliposomea mtihani wa Cambridge School Certificate.Alijiunga Makerere kusomea diploma katika afya ya wanyama.

Alipofika Makerere, Kibaki hakukaa sana kwa sababu aliondoka kuendelea na masomo London. Wekesa aliomba na kupata ufadhili wa masomo kusomea digrii ya afya ya wanyama katika chuo kikuu cha of Edinburgh, Scotland mwaka wa 1960; alihitimu mwaka wa 1966.

Wekesa alihudumu kama waziri wa Sayansi na Teknolojia na Misitu na Wanyamapori wakati wa utawala wa Kibaki wa mihula miwili baada ya kuhama chama cha Kenya African National Union (KANU) na kujiunga na siasa za upinzani wakati huo, wanasiasa walikuwa wakiungana kuondoa Moi mamlakani. Walikuwa wakijaribu kuunganisha Simeon Nyachae, Charity Ngilu, Michael Kijana Wamalwa na Kibaki, wote waliokuwa wagombea urais kwenye uchaguzi mkuu wa 1997.

“Wote walitaka kuwa wagombea urais katika uchaguzi mkuu wa 2002,” asema Wekesa.

Hivi ndivyo Wekesa alijipata akiwa sehemu ya kundi la watu 12 wabunge na mashirika ya kijamii waliobuni National Alliance for Change (NAC).

Mwaka huo alichaguliwa mwenyekiti wa kamati shirikishi ya NAC na pia akawa kaimu mwenyekiti wa baraza la chama cha National Alliance Party of Kenya. Alikuwa mmoja wa wazee 10 waliofanikisha kuundwa kwa muungano wa National Alliance Rainbow Coalition NARC.

Je, daktari wa afya wanyama aliwezaje kujiunga na siasa? Baada ya kurudi Kenya kutoka Chuo Kikuu cha Edinburgh, Wekesa alijiunga na Wizara ya Kilimo na Mifugo kama Afisa wa Afya ya Wanyama huko in Ol Kalou, kisha zilizokuwa wilaya za South Nyanza na Kisii kabla ya kupandishwa cheo kuwa Mkuu wa Afya ya Wanyama katika mkoa wa Nyanza.Akiwa Ol Kalou, alitangamana na mbunge wa eneo hilo, marehemu J.M. Kariuki.

Ni akiwa Homa Bay mwaka wa 1967 ambapo alikutana na Moi kwa mara ya kwanza akiwa makamu wa rais wakati huo katika ziara ya kukagua miradi ya serikali.

Mwaka wa 1969 alijiuzulu kazi ya serikali na kuanza yake ya huduma za afya ya wanyama Kitale ambapo wakazi walimwendea na kumshawishi agombee kiti cha ubunge cha Kitale West mwaka wa 1983. Alishindwa na kurudia kazi yake. Alishinda katika uchaguz mkuu wa 1988 na kuwa mbunge wa kwanza wa eneobunge la Kwanza.

  • Tags

You can share this post!

Migogoro: Korti yasimamisha uchaguzi katika kamati ya...

DARUBINI YA WIKI, Toleo Nambari 07, Oktoba 16, 2022

T L