• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 6:55 AM
BENSON MATHEKA: Uchaguzi mkuu sio mzaha, tujitokeze kwa wingi kupiga kura tupate viongozi wema

BENSON MATHEKA: Uchaguzi mkuu sio mzaha, tujitokeze kwa wingi kupiga kura tupate viongozi wema

NA BENSON MATHEKA

SIKU kama ya leo wiki ijayo Agosti 9, Wakenya watafanya uamuzi muhimu kwa kushiriki uchaguzi mkuu.

Watakuwa wakichagua viongozi wao kwa miaka mitano ijayo akiwemo rais wa tano.

Ni shughuli isiyokuwa na mzaha kwa kuwa itaamua mwelekeo ambao nchi itachukua.

Suala la uchaguzi mkuu si la kuchukuliwa kwa urahisi au kupuuzwa jinsi baadhi ya watu wanavyofanya.

Serikali ijayo iko mikononi mwa zaidi ya wapigakura milioni 22 ambao wamesajiliwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).

Hapa kuna mambo mawili; kukosa kujitokeza kupiga kura na kujitokeza kupiga kura.

Kukosa kujitokeza kutaamanisha kuwa unakubali yeyote atakayechaguliwa na sera zake bila kujali athari zake kwa nchi na kwako binafsi.

Wanaofanya hivyo hawafai kulalamika viongozi wabaya wakiingia madarakani.

Hata hivyo, wao ndio huwa wanalalamika zaidi mambo yanapoenda kombo wakilaumu viongozi kwa sera zao.

Kama wangejitokeza, pengine kura yao moja, ingeleta mabadiliko makubwa kwa mwelekeo wa nchi.

Wanaojitokeza kupiga kura huwa na sababu ya kuwakosoa viongozi waliowachagua wakienda kinyume na viapo vya ofisi au wasipotimiza ahadi wanazowapa wakati wa uchaguzi mkuu.

Hii ni kwa sababu huwa wana ujasiri wa kutekeleza haki yao ya demokrasia. Haki hii haihitaji woga; woga ni adui wa demokrasia.

Msingi wa demokrasia ni wengi wape na wachache kubaki watazamaji hata kama ndio wenye haki.

Wengi wakichagua viongozi wabaya kwa sababu ya kujitokeza kwa wafuasi wa wale wazuri, nchi huwa inatumbukia kwenye shida huku kila mmoja akiumia.

Njia ya kuepuka hali hii ni kuwa na ujasiri wa kujitokeza kupiga kura kushiriki katika kuamua serikali ijayo.

  • Tags

You can share this post!

PSG yakomoa Nantes na kujizolea taji la Trophee des...

Ramsey apata hifadhi mpya katika klabu ya Nice nchini...

T L