NA BENSON MATHEKA
WITO wa Rais William Ruto kwa Wakenya kulipa ushuru unafaa kuzingatiwa na kila mtu bila kujali tabaka lake.
Hii ni kwa sababu kuna tabaka la watu wanaotumia njia za mkato kuepuka kulipa ushuru unaostahili.
Hawa ni watu ambao huwa na ushawishi mkubwa serikalini na ndio wanafaa kumulikwa sana.
Kuna watu wanaojulikana kwa utajiri mkubwa nchini kwa sababu hawalipi ushuru na hawa hawafai kusamehewa.
Hebu tafakari kuhusu mtu anayesafiri kupitia barabara zilizojengwa kwa ushuru wa Sh20 ambao Mkenya wa kawaida anatoa huku akinyima serikali Sh2 milioni kutoka kwa kandarasi ambayo amepatiwa na serikali iyo hiyo.
Bwanyenye kama huyo anapitia barabara hizo akielekea uwanja wa ndege kwenda ng’ambo kutafuta matibabu kwa kuwa hospitali za serikali ya Kenya hazina dawa kwa sababu amekataa kulipa ushuru.
Japo Rais Ruto anasisitiza kuwa Wakenya hawafai kuhangaishwa wakidaiwa ushuru, kuna haja ya mikakati ya kuhakikisha wanaokataa kufanya hivyo makusudi wanachukuliwa hatua za kisheria.
Kulegeza mchakato wa kulipa ushuru kunaweza kuwa na athari hasi hata wakati mbinu zinawekwa kuvutia na kuongeza idadi ya watu wanaolipa ushuru.
Himizo liwe kwa kila mtu na sio makosa kukumbusha wanaokataa kufanya hivyo kupitia njia za kisheria.
Matajiri wanapokosa kulipa ushuru wa utajiri wanaomiliki, mzigo huwa unatwikwa maskini ambaye tayari analemewa na mlima wa ushuru na ada mbali mbali anapohitaji huduma kutoka kwa idara na ofisi za serikali.
Kulipa ushuru ni kujitegemea lakini kuachia mahasla ulipaji wa ushuru wakati matajiri wanakwepa ni kupalilia umaskini hasa pale ushuru huo unalenga rasilmali haba za ardhi wanazorithi.
Subscribe our newsletter to stay updated