NA CECIL ODONGO
WIKI jana, Kiongozi wa Upinzani Raila Odinga alitoa tathmini yake kuhusu utendakazi wa Rais William Ruto kwa muda wa siku 100 tangu achukue usukani baada ya uchaguzi wa Agosti 9.
Kwa kiasi fulani, tathmini ya Bw Odinga inalenga ndipo kwa sababu ni dhahiri kuwa utawala wa Kenya Kwanza umeanza kujikokota au kughairi nia kuhusiana na ahadi nyingi ilizotoa kwa raia wakati wa kampeni
Nashawishika kusema kuwa nyingi za ahadi ambazo Rais Ruto alikuwa akitoa katika majukwaa mbalimbali huenda hazitatekelezwa hata miaka mitano ijayo iwapo baada ya siku chache tu, ameanza kulalamika na kukasirika kuwa anashinikizwa na upinzani.
Uongo mkubwa ambao Rais aliwapa Wakenya ni kuwaambia kuwa kufikia mwanzo wa Disemba 2022, kila mmoja wao angekuwa na Bima ya Kitaifa ya Afya (NHIF).
Rais alitoa ahadi hiyo katika mkutano wa kampeni kule Ndia, Kaunti ya Kirinyaga mnamo Februari.
Kutotimizwa kwa ahadi hiyo kunaonyesha kuwa wanasiasa huwa radhi kusema tu kitu mradi wapate kura na kufanikiwa kuingia mamlakani.
Wakenya nao hawajifunzi lolote na huwashabikia wanasiasa bila kuweka kwenye mizani uhalisia wa ahadi zinazotolewa.
Hivi majuzi tu wakati wa kampeni ya uchaguzi mdogo katika Kaunti ya Bungoma, mmoja wa wawaniaji wa Useneta alipigiwa makofi na kushangiliwa akiwaambia wananchi kuwa akichaguliwa, atahakikisha kuwa anawajengea barabara na bwawa.
Kwenye katiba, kazi ya Seneta ni kutunga sheria na kupitisha miswada ambayo inaongoza utendakazi wa idara mbalimbali za serikali.
Katika kisa cha Bungoma, tamko la mwaniaji huyo lingekuwa na uhalisia iwapo angetoa pesa hizo mwenyewe kugharimia ujenzi wa barabara na bwawa, jambo ambalo pia ni nadra sana miongoni mwa wanasiasa wetu.
Ahadi sawa na hizo ndizo zilishamiri wakati wa kampeni za mirengo ya Kenya Kwanza na Azimio la Umoja ndiposa baada ya Rais Ruto kuchaguliwa, ameanza kupata ugumu na kutapatapa katika kutekeleza ahadi alizotoa.
Haitashangaza kuwa katika uchaguzi wa 2027, utawala wa sasa utarejea kwa Wakenya na ahadi zile zile ambazo ulitoa kwenye kampeni za 2022 na Wakenya bado watawapigia makofi wanasiasa wanaoegemea huko na kuwachagua tena.
Kila anapopanda jukwaani, Rais Ruto amekuwa akilalamika kuwa alirithi uchumi ambao umesambaratika kutokana na siasa za handisheki kati ya Bw Odinga na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta.
Kinaya ni kwamba bei ya bidhaa za kimsingi kama vile mafuta, unga na kwa ujumla gharama ya maisha imepanda sana kuliko siku za mwisho za utawala wa Rais Kenyatta.
Mwezi ujao – Januari 2023 – watoto watakuwa wakirejea shuleni na ukiangalia mwongozo wa kulipa karo, pesa ni za juu baada ya ufadhili wa serikali kuondolewa.
Je, hili pia linahitaji subira na Rais kutoshinikizwa?
Kuondoa ufadhili wa unga, mafuta na ufadhili wa elimu tayari kunawaumiza wazazi wengi na ungefanywa kwa mpango.
Aidha ni vigumu kuhisi kuwa uongozi huu wa Kenya Kwanza upo mamlakani na unawajibikia raia kwa kuwa hata katika mikutano ya umma wanayoihutubia, ahadi hutolewa ilhali haifahamiki kuwa zitatekelezwa lini.
Wakenya wajikaze na kufunga mikanda maisha yanapoendelea kuwa magumu ila kuna uwezekano finyu kuwa mambo yatabadilika siku za usoni.
Subscribe our newsletter to stay updated