• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 6:09 PM
ONYANGO: Mchujo ufanywe siku moja kubana nje wanaorukaruka

ONYANGO: Mchujo ufanywe siku moja kubana nje wanaorukaruka

Na LEONARD ONYANGO

PENDEKEZO la Msajili wa Vyama vya Kisiasa, Bi Anne Nderitu, kwamba vyama vya kisiasa viandae kura za mchujo siku moja ili kufungia nje wanasiasa walio na mazoea ya kuruka kutoka chama kimoja hadi kingine baada ya kubwagwa, linafaa kuungwa mkono.

Hatua ya wanasiasa kukimbilia vyama vingine baada ya kushindwa katika kura za mchujo, imetia doa siasa za humu nchini.

Kufanyika kwa mchujo siku moja kutapunguza joto la kisiasa ambalo huletwa na kura hizo katika baadhi ya maeneo nchini.

Japo wanasiasa hao wana uhuru wa kisiasa wa kujiunga na chama chochote wapendacho, kutangatanga huko baada ya kubwagwa ni ithibati tosha kwamba siasa za humu nchini hazijakomaa na wanasiasa wanaongozwa masilahi yao ya kibinafsi na wala si sera.

Ulafi huo ndio umefanya karibu kila mwanasiasa anang’ang’ania kuunda chama chake.Kufikia sasa, Kenya ina vyama vya kisiasa 75 ambavyo vimesajiliwa kikamilifu.

Vyama 10 vimetuma maombi ya usajili na vingine 22 vimepewa cheti cha muda vikiendelea na harakati za kusajiliwa kikamilifu.Chama kinafaa kuongozwa na sera na wala si uchu wa vyeo.

Kwa mfano, hakuna tofauti ya sera baina ya chama cha ODM chake Raila Odinga na United Democratic Alliance (UDA) cha Naibu wa Rais William Ruto.

Ni vigumu kutofautisha sera zao ambazo wamekuwa wakieleza Wakenya katika kampeni zao ambazo wamekuwa wakifanya katika maeneo mbalimbali nchini.

Bw Odinga akiondoka ODM huo ndio utakuwa mwisho wa chama cha Chungwa kwani wanachama wote wataondoka na kumfuata anakoenda.

Kadhalika, Dkt Ruto akiondoka UDA, huo ndio utakuwa mwisho wa chama hicho cha Wilibaro.

Wanasiasa wanaodai kuwa wanachama wa UDA hawaamini chochote ndani ya chama hicho. Hiyo ndiyo maana mbunge wa Kandara Alice Wahome, miezi michache iliyopita alishindwa kuelezea maana ya mfumo wa ‘Bottom Up’ ambao Dkt Ruto amekuwa akidai kuwa utaangamiza umaskini unaohangaisha zaidi ya asilimia 90 ya Wakenya.

Katika ripoti yake iliyotolewa hivi karibuni, Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) pia inalalamikia idadi kubwa ya wawaniaji wa kujitegemea kama moja ya changamoto kuu zinazotatiza maandalizi yake.

Katika uchaguzi wa 2017, wawaniaji 3,752 wa kujitegemea waliwania viti mbambali kama wagombea wa kujitegemea. Kati yao 2,918 waliwania udiwani huku 605 wakigombea ubunge.

Lakini idadi kubwa ya wawaniaji hao wa kujitegemea waligura vyama baada ya kushindwa katika kura za mchujo.Kuna haja ya kubadilisha sheria itakayozuia wanasiasa kuhama vyama vyao mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu ili kudumisha nidhamu vyamani.

Wanaotaka kuwania kama wagombea wa kujitegemea pia wanafaa kutangaza msimamo mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu.

  • Tags

You can share this post!

WARUI: Tuzo ya Nobel ya Abdulrazak ushindi kwa elimu Afrika

‘Kenya imefanikiwa kuwakabili kikamilifu nzige...

T L