RIPOTI ya hivi punde iliyotayarishwa na afisi ya Msimamizi wa Bajeti (CoB) Margaret Nyakango inasema kuwa kaunti zote 47 zinadaiwa jumla ya Sh105 bilioni na wanakandarasi na wafanyabiashara huku zikisalia siku 48 kabla ya uchaguzi mkuu kuandaliwa.
Kulingana na ripoti hiyo, magavana 11 kati ya 21 ambao wanahudumu muhula wa pili na wa mwisho, ni miongoni mwa wale ambao wanadaiwa kiasi kikubwa cha fedha na wanakandarasi.
Kwa mfano, kaunti za Narok, Mombasa, Embu, na Murang’a ni miongoni mwa kaunti zinazozongwa na malimbikizo ya madeni ya karibu Sh2 bilioni, kila moja.
Tusije tukasahau kuwa tangu Juni 2019, Rais Uhuru Kenyatta amekuwa akizitaka asasi zote za serikali kuu na zile za kaunti kulipa madeni yote yaliyothibitishwa kuwa halali.
Isitoshe, akisoma bajeti ya mwaka wa kifedha wa 2022-2023 bungeni mnamo Aprili 7, Waziri wa Fedha Ukur Yatani iliwahimiza magavana kulipa malimbikizi ya madeni.