NA WANTO WARUI
HUKU mtihani wa Kidato cha Nne (KCSE) ukielekea kumalizika, matokeo ya mtihani wa Darasa la Nane, KCPE, yanatarajiwa kutangazwa wakati wowote juma hili na Waziri wa Elimu Ezekiel Machogu.
Wazazi na wanafunzi zaidi ya milioni moja waliofanya mtihani huo wanasubiri matokeo hayo kwa hamu kubwa.
Aidha, walimu nao wanayangojea matokeo kwa mseto wa furaha na wasiwasi wakitarajia wanafunzi waliowanoa kufanya vyema.
Aghalabu, baada ya matokeo ya mtihani kutangazwa, kuna wale hushangilia kutokana na kufuzu kwa wana wao. Wengi hujibwaga barabarani kwa sherehe.
Bila shaka kuna wale huangaziwa na vyombo vya habari baada ya kuzoa alama za juu.
Shamrashamra za hapa na pale hujaa kote nchini. Hata hivyo,kuna wanafunzi ambao hawabahatiki kupata alama ambazo walikuwa wakitarajia.
Baadhi yao husononeka kiasi cha kutamauka maishani. Kuna wale huhimili vishindo vya kejeli na aibu kutoka kwa majirani au maadui na kuna wale ambao mioyo yao ni miepesi ya kuweza kudhibiti masimango ya wasiowapenda.
Kumekuwa na habari kuwa, kuna idadi fulani ya wanafunzi ambao hupatwa na shinikizo la mawazo na hata wengine kujitoa uhai kwa sababu ya matokeo duni.
Visa kama hivi vimekuwa vikiripotiwa mara kwa mara kutoka sehemu mbalimbali nchini.
Hakuna sababu yoyote ambayo inaweza kusababisha mwanafunzi ajitoe uhai kwa sababu ya mitihani isipokuwa kukosa kuelekezwa vyema kwamba kufeli mtihani sio mwisho mwa maisha.
Wazazi wana jukumu kubwa la kuwatayarisha kimawazo kabla matokeo ya mtihani hayajatangazwa ili wawe tayari kupokea matokeo yoyote yale kwa ujasiri.
Baadhi ya wazazi huwatayarisha watoto vibaya kwa kuwatia hamu kuu kuwa watapata alama za juu.
Alama hizo zinapokosekana, mtoto huyo hana jingine ila kuzama kwenye mawazo yasiyofaa.
Subscribe our newsletter to stay updated