• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
AC Milan warejea kileleni mwa jedwali la Serie A

AC Milan warejea kileleni mwa jedwali la Serie A

Na MASHIRIKA

AC Milan walirejea kileleni mwa jedwali la Ligi Kuu ya Italia (Serie A) baada ya kutandika Cagliari 1-0 mnamo Jumamosi usiku.

Bao la pekee katika mchuano huo lilijazwa kimiani na nyota wa Algeria, Ismael Bennacer aliyekamilisha krosi ya Olivier Giroud katika dakika ya 59. Leonardo Pavoletti nusura asawazishie Cagliari mwishoni mwa kipindi cha pili ila kombora lake likabusu mwamba wa goli.

Ilikuwa mara ya tatu mfululizo kwa Milan kusajili ushindi wa 1-0 katika Serie A. AC Milan kwa sasa wanaselelea kileleni mwa jedwali la Serie A kwa alama 66, tatu zaidi kuliko nambari mbili Napoli waliotoka nyuma na kutandika Udinese 2-1.

Udinese waliwekwa kifua mbele na Gerard Deulofeu kabla ya Napoli kusawazisha kupitia Victor Osimhen ambaye sasa anajivunia mabao manne kutokana na mechi mbili zilizopita.

Udinese walikamilisha mechi wakiwa na wachezaji 10 pekee uwanjani baada ya beki Pablo Mari anayewachezea kwa mkopo kutoka Arsenal kuonyeshwa kadi nyekundu mwishoni mwa kipindi cha pili.

Mabingwa watetezi wa Serie A, Inter Milan walilazimishiwa na Fiorentina sare ya 1-1 na kusalia katika nafasi ya tatu kwa alama 60, sita nyuma ya AC Milan. Nafuu zaidi kwa Inter ni kwamba wana mchuano mmoja zaidi wa kutandaza ili kufikia idadi ya mechi 30 ambazo tayari zimepigwa na Napoli na AC Milan.

Lucas Torreira aliwaweka Fiorentina uongozini mwanzoni mwa kipindi cha pili kabla ya Denzel Dumfries kusawazishia Inter Milan.

MATOKEO YA SERIE A (Jumamosi):

Cagliari 0-1 AC Milan

Napoli 2-1 Udinese

Inter Milan 1-1 Fiorentina

You can share this post!

Jeraha kumkosesha kipa Ramsdale mechi mbili zijazo za...

Lewandowski aweka rekodi mpya ya ufungaji wa mabao...

T L