• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 8:55 PM
AK kutumia mchujo wa kitaifa mnamo Julai ugani Kasarani kuteua kikosi cha Riadha za Kimataifa kwa Chipukizi wa U-20

AK kutumia mchujo wa kitaifa mnamo Julai ugani Kasarani kuteua kikosi cha Riadha za Kimataifa kwa Chipukizi wa U-20

Na CHRIS ADUNGO

KENYA itatumia mchujo wa mbio za chipukizi wasiozidi umri wa miaka 20 mnamo Julai 2-3 ugani MISC Kasarani kuteua kikosi cha watimkaji 70 watakaopeperusha bendera ya Kenya kwenye Riadha za Dunia za U-20 mnamo Agosti 17-22, 20121 uwanjani Kasarani, Nairobi.

Kwa mujibu wa Barnaba Korir ambaye ni Afisa MKuu wa Shirikisho la Riadha la Kenya (AK), mchujo ujao wa kitaifa utakuwa jukwaa zaidi la kukadiria kiwango cha kujiandaa kwa chipukizi hao kwa mapambano hayo ya kimataifa.

Koriri amesisitiza kwamba maazimio yao ni kuandikisha matokeo bora zaidi kuliko yale yaliyosajiliwa na chipukizi wasiozidi umri wa miaka 18 kwenye Riadha za Dunia zilizoandaliwa pia ugani MISC Kasarani mnamo 2017.

Kenya ilikuwa iwe mwenyeji wa mbio hizo mnamo Julai 2020 ila zikaahirishwa kutokana na janga la corona. Korir amesema kusogezwa kwa tarehe ya kivumbi hicho kunatarajiwa kuwapa wanariadha wa Kenya fursa nzuri zaidi ya kujifua vilivyo kwa mashindano yenyewe.

“Mchujo wa Julai utatuchorea picha kamili kuhusu jinsi kikosi kimejiandaa. Vifaa vitakavyotumika kwenye majaribio ndivyo vitakavyotumika pia wakati wa Riadha za Dunia. Kwa hivyo, tutapata fursa nzuri ya kufahamu mapungufu yetu ili tujiimarishe zaidi na kuboresha kiwango cha maandalizi,” akasema kwa kusisitiza kwamba AK ilijifunza mambo mengi kutokana na maandalizi ya mbio za dunia za mabara almaarufu Kip Keino Classic mnamo Oktoba 2020.

Kwa upande wake, Afisa Mkuu Mtendaji wa Shirikisho la Riadha Duniani (WU), Mike Rabar, amesema kwamba uga wa Kasarani uko katika hali shwari japo zipo baadhi ya sehemu chache zitakazohitaji kukarabatiwa kabla ya Julai 2021.

Korir ambaye pia ni mkurugenzi wa AK anayesimamia masuala ya makuzi na maendeleo ya chipukizi, amesema mchujo ujao wa kitaifa utashirikisha wanariadha wataokuwa wamealikwa pekee.

Kikosi kitakachoteuliwa kitaingia kambini ambako kitasaidiwa kujiandaa kwa riadha hizo za kimataifa miongoni mwa chipukizi.

“Tofauti na hapo zamani, tutapunguza kabisa idadi ya kambi ambapo tutalenga zaidi kuwamakinikia wanariadha tutakaokuwa tumeteua pekee,” akasema Korir kwa kufichua kwamba kutakuwa na kambi itakayopigwa mnamo Aprili 2021 kabla ya kikosi cha mwisho kitakachowakilisha Kenya kuteuliwa na AK mwezi mmoja baadaye.

Hata hivyo, Korir ameshikilia kwamba kuahirishwa kwa riadha za kimataifa za chipukizi kutoka Julai 7-12 mwaka wa 2020 hadi mwaka wa 2021 kulifanya idadi kubwa ya watimkaji waliokuwa wawakilishe Kenya kukosa nafasi kwa sababu watakuwa wamepita umri wa kushiriki mashindano hayo.

Kwa mujibu wa kanuni mpya za mashindano ya U-20, wanariadha wenye umri wa miaka 16, 17, 18 au 19 kufikia Disemba 31, 2021 wataruhusiwa kushiriki.

“Tuna kinarua kigumu cha kuteua kikosi kipya kwa minajili ya mapambano yajayo ya riadha za chipukizi wa U-20 kwa sababu wengi waliofanyiwa mchujo hapo awali sasa wamepita umri wa kushirki,” akasema Korir.

Kwa mujibu wa kinara huyo, AK itapania kuwajibisha idadi kubwa ya wanariadha kwenye mbio fupi na za masafa ya kadri uwanjani.

“Tutategemea zaidi huduma za wakufunzi wetu akiwemo Andrew Martim ambaye alipokea mafunzo nchini Japan kuwanoa wanariadha wetu kwa minajili ya mbio fupi na za masafa ya kadri,” akasema Korir.

Kenya itawakilishwa kwenye fani 21 mbalimbali kati ya 22 zitakazoshindaniwa kwenye riadha hizo za chipukizi kwa upande wa wavulana na wasichana. Kitengo cha pekee ambacho kitashuhudia Kenya ikikosa mwakilishi ni kuruka juu kwa kutumia ufito.

Kenya ilitwaa ubingwa wa mwaka wa 2018 kwenye riadha hizo za chipukizi baada ya kujizolea jumla ya nishani 11: sita za dhahabu, nne za fedha na moja ya shaba jijini Tampere, Finland.

You can share this post!

Kenya Prisons na KCB waanza kujinoa kwa Ligi Kuu ya...

Kuco yadai CoG ilihepa wakati wa kutia saini makubaliano ya...