• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 3:07 PM
Barcelona waafikiana na Bayern kuhusu uhamisho wa Robert Lewandowski hadi Camp Nou

Barcelona waafikiana na Bayern kuhusu uhamisho wa Robert Lewandowski hadi Camp Nou

Na MASHIRIKA

BARCELONA wameafikiana na Bayern Munich kuhusu uhamisho wa fowadi matata raia wa Poland, Robert Lewandowski hadi uwanjani Camp Nou.

Nyota huyo mwenye umri wa miaka 33 angali na miezi 12 zaidi kwenye mkataba wake wa sasa na Bayern. Hata hivyo, aliwaambia miamba hao wa Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga) mnamo Juni 2022 kwamba alitaka kuondoka na kuelekea kwingineko.

Lewandowski alifunga mabao 50 kutokana na mechi 46 mnamo 2021-22 na kusaidia Bayern kunyanyua taji la Bundesliga kwa mara ya 10 mfululizo.

Sogora huyo alijiunga na Bayern bila ada yoyote mnamo 2014 baada ya kuagana rasmi na Borussia Dortmund. Tangu wakati huo, amefungia Bayern magoli 344 kutokana na mechi 374, matokeo yanayomweka katika nafasi ya pili nyuma ya marehemu Gerd Muller kwenye orodha ya wafungaji bora wa muda wote kambini mwa Bayern.

Lewandowski ameshinda taji la Bundesliga katika misimu yote minane ya kuhudumu kwake kambini mwa Bayern aliowasaidia pia kutwaa taji la Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo 2019-20 baada ya kukomoa Paris Saint-Germain (PSG) 1-0 jijini Lisbon, Ureno.

Bayern wametangaza pia kwamba fowadi mahiri raia wa Ujerumani, Serge Gnabry, 27, ametia saini mkataba mpya utakaomshuhudia sasa akihudumu ugani Allianz Arena hadi 2026.

Lewandowski atakuwa sogora wa nne kuingia katika sajili rasmi ya Barcelona muhula huu baada ya Raphinha Belloli, Franck Kessie na Andreas Christensen.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Mchezaji wa zamani wa Simba, Gor kunoa Meru Bombers

Namna tofauti za kukabili maumivu ya kichwa

T L