• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
Benzema afunga mabao mawili na kusaidia Real kukung’uta Shakhtar Donetsk kwenye UEFA

Benzema afunga mabao mawili na kusaidia Real kukung’uta Shakhtar Donetsk kwenye UEFA

Na MASHIRIKA

KARIM Benzema alifunga mabao mawili katika ushindi wa 2-1 uliosajiliwa na waajiri wake Real Madrid dhidi ya Shakhtar Donetsk ya Ukraine katika mchuano wa Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Jumatano usiku uwanjani Santiago Bernabeu, Uhispania.

Matokeo hayo yalipaisha Real ya kocha Carlo Ancelotti hadi kileleni mwa Kundi D kwa alama tisa, mbili zaidi kuliko nambari mbili Inter Milan waliokung’uta Sheriff Tiraspol 3-1 nchini Moldova. Shakhtar Donetsk wanavuta mkia kwa pointi moja, tano zaidi nyuma ya Sheriff wanaokamata nafasi ya tatu.

Benzema alipachika wavuni bao la kwanza katika 14 na hilo likawa bao la 1,000 kwa Real kufunga katika soka ya bara Ulaya. Benzema ambaye ni raia wa Ufaransa, alitikisa nyavu za wageni wao kwa mara nyingine katika dakika ya 61 baada ya kushirikiana vilivyo na Vinicius Junior na Casemiro. Shakhtar Donetsk walikuwa wamerejeshwa mchezoni na Fernando kunako dakika ya 39.

Real walishuka dimbani wakiwa na kiu ya kuendeleza ubabe wao dhidi ya Shakhtar Donetsk baada ya kupepeta kikosi hicho 5-0 katika mchuano wa mkondo wa kwanza wa Kundi D mnamo Oktoba 19, 2021.

Kiungo mzoefu raia wa Croatia, Luka Modric, alipoteza nafasi nyingi za wazi za kufungia Real mabao zaidi katika kipindi cha pili. Real kwa sasa wameshinda mechi nne mfululizo kati ya tano zilizopita katika mashindano yote.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Wakenya washauriwa wawe waangalifu machafuko yakishuhudiwa...

Fairtrade yakusanya sahihi 1.8 milioni za wakulima...

T L