Na GEOFFREY ANENE
TIMU ya Ionikos anayochezea Mkenya Abud Omar imepata pigo katika juhudi zake za kuingia Ligi Kuu msimu ujao baada ya kung’olewa kileleni mwa ligi ya daraja ya pili kwa kulimwa 2-0 na Xanthi, Jumapili.
Ionikos ilifanya vizuri katika msimu wa kawaida na kuumaliza katika nafasi ya kwanza kwa alama 47.
Ilifuatiwa na Xanthi (41), Levadiakos (41), Ergotelis (36), PAE Chania (35) na Diagoras (30) zote zikinyakua tiketi ya kuingia mchujo wa timu sita-bora ambapo mshindi atapandishwa daraja.
Tangu mchujo huo uanze, Ionikos haijapata hata alama moja. Ililemewa na Levadiakos 3-2 Aprili 28, PAE Chania 1-0 (Mei 5) na Xanthi 2-0 (Mei 9). Waliozamisha Ionikos siku ya Jumapili ni beki Mholanzi Daryl Werker na Mgiriki Athanasios Papazoglou. Walitikisa nyavu dakika ya 24 na 70, mtawalia.
Baada ya kuchapwa Jumapili, Ionikos imetupwa chini kutoka nafasi ya kwanza hadi nambari tatu. Xanthi inaongoza kwa alama 48 baada ya kuzoa alama saba katika mechi tatu zilizopita. Levadiakos ni ya pili kwa alama 47, mbele ya Ionikos kwa tofauti ya ubora wa magoli. Timu ya Levadiakos imechabanga Diagoras 4-0 Jumapili.