• Nairobi
  • Last Updated May 6th, 2024 1:13 PM
Dortmund yakung’uta Arminia na kukaribia Bayern Munich kileleni mwa Bundesliga

Dortmund yakung’uta Arminia na kukaribia Bayern Munich kileleni mwa Bundesliga

Na MASHIRIKA

CHIPUKIZI matata raia wa Uingereza, Jude Bellingham, alifunga bao kwa ustadi mkubwa katika dakika ya 72 na kusaidia waajiri wake Borussia Dortmund kucharaza Arminia Bielefeld 3-1 katika mechi ya Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga).

Tineja huyo mwenye umri wa miaka 18 aliokota mpira nje ya kijisanduku cha Arminia na kuwazidi ujanja mabeki watatu kabla ya kuelekeza kombora zito langoni. Mabao mengine ya Dortmund yalifumwa wavuni kupitia Emre Can na Mats Hummels. Wenyeji Arminia walifutiwa machozi na Klos katika dakika ya 87.

Dortmund kwa sasa wanashikilia nafasi ya pili jedwalini kwa alama 21, moja pekee nyuma ya viongozi Bayern Munich waliopepeta Hoffenheim 4-0.

Mshambuliaji na nahodha wa Poland, Robert Lewandowski alitumia mechi hiyo kufunga bao lake la 10 kutokana na mechi tisa zilizopita za Bundesliga akivalia jezi za Bayern waliofungua ukurasa wa mabao kupitia Serge Gnabry.

Eric Maxim Choupo-Moting na Kingsley Coman walikuwa wafungaji wengine wa mabao ya Bayern ambao ni mabingwa watetezi wa Bundesliga.

Bayern walijibwaga ugani kwa ajili ya mechi dhidi ya Hoffenheim baada ya kuchabanga Bayer Leverkusen 5-1 wikendi iliyopita katika mechi ya Bundesliga kisha kupepeta Benfica 4-0 katika mchuano wa Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Oktoba 20, 2021.

Kocha Julian Nagelsmann wa Bayern alikosa mechi hiyo kwa kuwa yuko karantini baada ya kuambukizwa virusi vya corona.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Wazee wakemea viongozi kunyamazia mzozo kuhusu bahari

Ruto awarai vijana kutotumiwa kuzua ghasia

T L