NA MASHIRIKA
LONDON, Uingereza
BAADA ya kupoteza mechi zao za debi mwishoni mwa wiki, Manchester City na Tottenham Hotspur watashuka leo Alhamisi ugani Etihad kila mmoja akilenga kutamalaki gozi hilo la Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).
Man-City wanaonolewa na Pep Guadiola walichapwa 2-1 na Manchester United ugani Old Trafford mnamo Jumamosi, siku moja kabla ya Spurs kupigwa na Arsenal 2-0 mbele ya mashabiki wa nyumbani.
Guardiola amesema mawazo yake hayako kwa ubingwa wa EPL msimu huu, ingawa kikosi chake kinaendelea kutia Arsenal ya kocha Mikel Arteta kileleni mwa jedwali.
Kufikia sasa, mabingwa watetezi wa EPL, Man-City, wanakamata nafasi ya pili jedwalini kwa alama 39, nane nyuma ya Arsenal ambao pia wametandaza mechi 18.
Kwa upande wake, kocha Antonio Conte wa Spurs amesema hafai kulaumiwa kutokana na matokeo duni ya timu hiyo.
Conte amedai kuna watu wengine wanaopaswa kubeba mzigo huo wa lawama baada ya timu kushindwa mara tano katika mechi tisa ligini.
Licha ya Spurs kushuka hadi nafasi ya tano jedwalini, Conte amesisitiza kuwa hajaona maafisa wengine wa klabu hiyo wakiwemo madaktari na wakurugenzi wa idara ya michezo wakilalamika kuhusu mfumo unaotumiwa kwa sasa.
“Nchini Italia, kabla ya mechi kuanza, kuna mtu anayezungmza na waandishi wa habari. Hapa pia inafaa iwe hivyo, lakini imekuwa ni mimi tu ninayeeleza kila kitu, hivyo sioni kama ni sawa.”
“Wakati umefika kwa wakuu wa klabu kuwakilishwa katika mikutano ya pamoja na waandishi wa habari kueleza kinachoendelea kikosini kwa sasa, la si hivyo, itaonekana kuna jambo linalofichwa, ambalo linaendelea kutuvuruga,”akaelezea.
Spurs wameokota pointi 10 pekee kutokana na mechi tisa zilizopita.
Pengo la alama tano linatamalaki kati yao na Manchester United na Newcastle United amabo wametandaza mchuano mmoja wa ziada.
“Nionavyo, kila mtu anatia bidii uwanjani, lakini imekuwa vigumu kushinda. Kibarua ni kizito na matarajio ni mengi,” alisema kocha huyo wa zamani wa Chelsea.
Subscribe our newsletter to stay updated