• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 8:57 PM
Fursa ya Olunga kung’ara Kombe la Dunia la Klabu ni leo

Fursa ya Olunga kung’ara Kombe la Dunia la Klabu ni leo

Na GEOFFREY ANENE

Mshambuliaji matata Michael Olunga ana fursa kubwa ya kung’ara wakati wenyeji Al Duhail watafungua kampeni yao ya Kombe la Dunia la Klabu dhidi ya mabingwa wa Afrika Al Ahly nchini Qatar mnamo Alhamisi usiku. Mechi hiyo ya kufa-kupona ni ya raundi ya pili.

Olunga maarufu kama “Engineer” alikuwa na mwaka 2020 wa kufana alipofungia Kashiwa Reysol mabao 28 akiibuka mchezaji bora na mfungaji bora kwenye Ligi Kuu ya Japan.

Alijiunga na Al Duhail wiki moja baada ya msimu wa Japan kukatika Januari 4 na tayari amechezea mabingwa hao wa Qatar michuano mitatu. Alitangaza kilichofanya Al Duhail kumtafuta alipopachika mabao matatu katika ushindi wa mabao 6-0 dhidi ya Al Ahli Doha kwenye Kombe la Amir katika mechi ya mwisho ya klabu hiyo kabla ya kuzamia maandalizi ya mashindano hayo ya dunia.

Katika mahojiano ya awali, Olunga alifichua kuwa uweledi wake wa kutikisa nyavu ulisukuma Al Duhail kumnyakua kwa donge nono kutoka Japan.

“Kila mtu hapa anaamini katika uwezo wangu wa kuchangia katika mashambulizi nikishirikiana na wenzangu na hiyo ndiyo sababu maalum nililetwa hapa. Uwanjani, sote tunasaidiana na mashindano haya ni fursa nzuri kwetu sote. Kivyangu, nitajitahidi kufanya vyema.”

“Ni changamoto kwa kila mtu na tuko tayari kusakata mechi na kukabiliana na changamoto zilizo mbele yetu,” alisema Mkenya huyo mwenye umri wa miaka 26.

Pamoja na mchezaji bora wa Kombe la Bara Asia 2019 na mfungaji bora Almoez Ali na kiungo Edmilson Junior, ambaye amecheka na nyavu mara tano na kumega pasi nne zilizozalisha mabao katika michuano minane ya ligi msimu huu, watakuwa wachezaji tegemeo katika kambi ya Al Duhail.

Kupata mafanikio katika mashindano haya, washiriki wapya Al Duhail watahitaji kuwa makini na wachezaji matata wa Al Ahly kama Hussein Shehat, Kahraba na Mzambia Walter Bwalya. Mohamed El Shenawy aliibuka kipa bora kwenye Ligi Kuu ya Misri msimu 2019-2020 akimaliza mechi 25 bila kufungwa bao kwa hivyo haitakuwa kazi rahisi kwa wapinzani. Al Ahly wana uzoefu kutokana na kuwa walishiriki makala ya mwaka 2005, 2006, 2008, 2012 na 2013.

Mechi kati ya Al Duhail na Al Ahly itatanguliwa na washiriki wapya Tigres UANL kutoka Mexico (washindi wa Amerika ya Kaskazini, Kati na Caribbean) na mabingwa wa Bara Asia Ulsan Hyundai kutoka Korea Kusini itakayochezewa uwanjani Ahmed bin Ali saa kumi na moja jioni Februari 4. Mshindi kati ya Al Duhail na Al Ahly atamenyana na mastaa wa Bara Ulaya na Ujerumani Bayern Munich katika nusu-fainali Februari 7.

Wafalme wa Amerika Kusini Palmeiras kutoka Brazil wanasubiri mshindi kati ya Tigres na Ulsan katika nusu-fainali. Mashindano haya, ambayo hayana mwakilishi kutoka eneo la Oceania baada ya Auckland City kujiondoa kutokana na masharti makali ya kudhibiti virusi vya corona nchini mwao New Zealand, yatakamilika Februari 11. 

  • Tags

You can share this post!

Ulinzi Stars kutumia uwanja mbadala Afraha Stadium...

Mamia ya wakazi Mukuru kupoteza makao kupisha ujenzi wa...