NA RICHARD MAOSI
Timu ya wanajeshi ya Ulinzi Stars inayoshiriki ligi ya FKF nchini, italazimika kugura uwanja wa nyumbani Afraha Stadium unapoanza kukarabatiwa.
Operesheni hiyo itachukua zaidi ya miezi 14, kabla ya ratiba ya mechi za kawaida kurejea, hii ikiwa ni mojawapo ya mbinu za kuhakikisha Afraha inafikia hadhi za kimataifa.
Timu nyingi zimekuwa zikipata changamoto wakati wa mechi au kufanya mazoezi kutokana na hali duni ya uwanja.
“Uwanja wa Afraha unaweza kubeba zaidi ya mashabiki 8200, lakini ni wakati mwafaka wa kuimarisha viwango,”usimamizi wa kaunti ya Nakuru ulitangaza kupitia mtandao wa kijamii.
Afraha stadium itakuwa na chumba cha kufanyia mazoezi, kidimbwi cha kuogelea, vyumba vya kubadilisha , vyoo na sehemu ya kubarizi.
Kufikia mwaka wa 2022 uwanja wa Afraha utakuwa umepata sura mpya endapo serikali ya kaunti itajizatiti kuharakisha ukarabati.
Mradi huu unafadhiliwa na Kenya Urban Support programme, ambao umehasisiwa na benki ya dunia.
Katika awamu ya kwanza Afraha itamudu kubeba zaidi ya mashabiki 20,000 ambapo shilingi milioni 650 zinatarajiwa kutumika.
Uwanja wa Afraha utaanza kuandaa mashindano mengine mengi mbali na kabumbu, ili kukuza talanta za wanamichezo mashinani.
James Angila mkufunzi wa Nakuru All Stars anasema, hali nzuri ya uwanja itasaidia kuwavutia mashabiki hususan wakati wa mvua ambapo baadhi yao wamekuwa wakinyeshewa.
Kulingana naye ni mwamko mpya katika jumuia ya michezo , kwani uwanja wa Afraha utaanza kuandaa mechi za kimataifa
Hili linajiri baada ya baadhi ya viwanja kufanyiwa ukarabati kama vile Nyayo Stadium,na uwanja wa Ruaraka unaoandaa mechi za Tusker FC.