• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 10:50 AM
Ganda la muwa la vigongo westham anayeng’aria Ajax

Ganda la muwa la vigongo westham anayeng’aria Ajax

NA GEOFFREY ANENE

KIGOGO Sebastien Haller ni mmoja wa washambuliaji katili barani Ulaya.

Weledi wake langoni umeshuhudia akiongoza kampeni za kutwaa kiatu cha dhahabu kwenye Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) kwa mabao 10.Magoli hayo ni moja zaidi ya mfungaji bora wa msimu 2020-2021 Robert Lewandowski, baada ya mechi za makundi kukamilika.

Mohamed Salah (Liverpool) na Cristiano Ronaldo (Manchester United) wametikisa nyavu mara saba na sita mtawalia. Haller alisukumwa katika fani ya judo mapema maishani mwake.Mamake alipenda judo baada ya Ufaransa kufana katika miereka hiyo kwenye Olimpiki za 1996.

Hata hivyo, Haller hakupenda judo. Mwaka 2010 alitupilia mbali fani hiyo na kufuata ndoto yake: soka. Alipitia mikononi mwa Vigneux (2003-2005), Bretigny Foot (2005-2007) na Auxerre (2007-2012). Akiwa akademia ya Auxerre alijinadi wakati wa Kombe la Dunia la Chipukizi U-17 akichezea Ufaransa.

Wiki chache baada ya dimba hilo, akasaini kandarasi ya kwanza ya soka ya malipo akiwa Auxerre. Alifungia timu ya pili ya Auxerre mabao 29 katika mechi 57 msimu 2012-2013. Mnamo Julai 27,2012, alisakata mchuano wake wa kwanza wa Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1).

Muda si muda akatwaliwa na Utrecht mnamo Desemba 2014, akiifungia mabao 11 katika michuano 17 msimu wa kwanza. Alichangia magoli 30 katika mechi 65 msimu uliofuata kabla kunyakuliwa na Eintracht Frankfurt ya Ujerumani kwa mkataba wa miaka minne mnamo 2017.

Baada ya kung’ara Frankfurt na kuisaidia kufika nusu-fainali ya Uropa League, West Ham ilimsajili kwa Sh6.7 bilioni. Yeye ni mchezaji ghali kuwahi kununuliwa na West Ham. Ila hakufanya vyema jijini London. Akapata fursa ya kujifufua Ajax ilipomnunua kwa takriban Sh2.9 bilioni.

Akawa pia mchezaji ghali zaidi kuwahi kununuliwa na miamba hao wa Uholanzi.Tangu Novemba 2020, Haller anachezea Ivory Coast kimataifa. Mchezo wake unakaribiana na Mfaransa David Trezeguet. Ameoa na amejaliwa mtoto kwa jina Ciara Haller. Ametinga mabao tisa katika mechi 15 ligini msimu huu.

You can share this post!

Idara ya Utabiri wa Anga yaonya kuhusu mafuriko

Bwana ‘misuli’ maarufu Mr Kenya!

T L