IMETAYARISHWA NA CECIL ODONGO
KOCHA wa Crystal Palace Patrick Viera amesisitiza kuwa nyota wake Wilfried Zaha hatahamia Chelsea au Arsenal hivi karibuni kwa kuwa lengo lake ni kutambisha timu hiyo kutwaa mataji mengi.
Kulikuwa na ripoti kuwa Zaha alikuwa tayari kubanduka Selhurst Park na kuelekea Chelsea au Arsenal lakini uhamisho huo haukufanyika kabla ya makataa ya mnamo Alhamisi.
“Zaha anamakinikia kusalia hapa timuni na lengo lake ni kushinda mataji. Jinsi ninavyoona anavyojituma, ni wazi kuwa nia yake si kuhamia timu yoyote bali kuitumikia Crystal Palace,” akasema Viera, mchezaji wa zamani wa Arsenal.
Zaha, 29, raia wa Ivory Coast ameshaanza kuwa moto wa kuotea mbali sana msimu huu huku akifunga mabao matatu katika mechi tatu alizowajibikia waajiri wake.
Arsenal ilikuwa ikiwinda Zaha baada ya kumkosa 2019 lakini juhudi zao zilikosa kuzaa matunda kwa mara nyingine.