NA TOTO AREGE
WACHEZAJI 23 wa timu ya taifa ya Kenya Harambee Starlets, wameondoka nchini Jumanne kuelekea mjini Yaounde, Cameroon kumenyana na Indomitable Lionesses katika raundi ya kwanza kufuzu kwa Kombe la Afrika kwa Wanawake (WAFCON) 2024.
Mechi hiyo kali itasakatwa Ijumaa.
Kikosi hicho chini ya kocha Beldine Odemba, kina mchanganyiko wa wachezaji wanaokipiga nyimbani na wale ambao wanacheza soka ya kulipwa katika mataifa tofauti tofauti.
Cameroon imeorodheshwa katika nafasi ya tatu Afrika na ya 56 duniani huku Kenya ikishikilia nafasi ya 28 Afrika na 147 duniani.
Akizungumza baada ya mazoezi Jumatatu wiki hii ugani Kasarani Annex jijini Nairobi kabla ya kuondoka nchini, mshambulizi Mwamahalima ‘Dogo’ Jereko, alisema soka imebadilika na wenyeji Cameroon watapata wakati mgumu mbele ya mashabiki wao.
“Maandalizi tumefanya kama timu ingawa nilifika kuchelewa kutokana na shughuli za klabu lakini. Kulinganna na jinsi nimeona wachezaji, wako tayari kupigania taifa. Soka ni ile ile na wachezaji ni wale. Cha msingi ambacho tutafanya ni kuwasiliana uwanjani na tutawanyoosha wapinzani,” alisema Dogo.
“Nimecheza soka ya kulipwa nje ya nchi kwa muda sasa na nimejifunza kwamba, unaweza kucheza katika safu yoyotwe uwanjani. Kwenye timu ya taifa nacheza kama mshambulizi lakini katika klabu yangu nacheza kama kiungo, Ilikuwa vigumu mwanzoni lakini nilizoea,” aliongezea Dogo.
Kikosi kilichosafiri;
Makipa
Valentine Kwaka, Annedy Kundu na Caroline Rufa.
Mabeki
Phoebe Owiti, Enez Mango, Wincate Kaari, Ruth Ingosi, Vivian Nasaka, Janet Moraa, Waganda Lydia Akoth na Juliet Auma
Viungo wa kati
Cynthia Shilwatso, Sheryl Angachi, Vivian Corazone, Mercyline Anyango na Mercy Njeri
Washambulizi
Jentrix Shikangwa, Elizabeth Wambui, Mwanalima, Esse Akida, Tereza Engesha, Violet Nanjala na Mercy Airo.