Na VICTOR OTIENO
WAGENI Nepal wametawazwa washindi wa mashindano ya kimataifa ya kriketi ya ODI wakisalia na mechi moja baada ya kubwaga Kenya kwa mikimbio 16 katika klabu ya Nairobi Gymkhana, Jumamosi.
Nepal walitawala mchuano wa kwanza kwa wiketi saba Ijumaa kwa hivyo wanaongoza msururu huo wa mechi tatu 2-0. Timu hizo zitakutana kwa mechi ya tatu hapo Jumatatu.
Mnamo Jumamosi, Nepal, ambao wanakamata nafasi ya 19 katika viwango vya ubora vya Baraza la Kimataifa la Kriketi (ICC) vya ODI, ilishinda zoezi la kurusha sarafu hewani kuanzisha mechi na kuamua kupiga mipira.
Waliandikisha mikimbio 230 ambayo Kenya ilishindwa kufikia. Kenya ilipata mikimbio 214 kutokana na ova 46.3 wakati wa zamu yao.
Mpigaji wa mipira Rakep Patel kutoka Kenya aliibuka mfungaji bora kwa mikimbio 82 kutokana na mipira 104.
Nahodha wa Nepal, Rohit Kumar alitawazwa mchezaji bora wa mechi alipozoa mikimbio 78 kutokana na mipira 95.
Nepal pia ilipepeta Kenya 3-2 katika mechi za Twenty20. Kocha wa Nepal, Prabhakar Manoj alisema kutwaa mataji ya T20 na ODI ni dalili nzuri kwa siku za usoni za kriketi ya taifa hilo kutoka Bara Asia.
TAFSIRI: GEOFFREY ANENE