Na GEOFFREY ANENE
WAKENYA Bernard Kipkirui na Beatrice Cheserek wametawala mbio za Vila de Santa Pola Half Marathon nchini Uhispania, Jumapili.
Kipkirui amekamilisha mbio hizo za kilomita 21 kwa dakika 59:44 akifuatiwa na Wakenya wenzake Nehemiah Kipyegon (saa 1:00:37), Alfred Lipchirchir (1:00:49), Edwin Kipruto (1:00:59) na Dominic Bett (1:01:05).
Cheserek aliyekamata nafasi ya nne mwaka 2022, aliibuka mshindi upande wa wanawake kwa saa 1:07:49 akifuatiwa na Mkenya mwenzake Cynthia Jepkogei (1:08:41), Muethiopia Aminet Hamed (1:09:01) na Mkenya Nancy Jepleting (1:10:48). Wakenya Felix Kibitok na Pauline Esikon walinyakua mataji mjini Santa Pola mwaka 2022, kumaanisha mataji hayo hayajatoka Kenya.
Hapo Januari 21, Wakenya Titus Kimutai na Agnes Keino walitawala mbio za Buriram Marathon kwa rekodi mpya za Buriram Marathon saa 2:08:57 na 2:28:08 mtawalia. Kimutai alifuatiwa na Muethiopia Fikadu Kebede (2:10:49) na Mkenya Benson Mwangi (2:11:24) naye Keino alimaliza mbele ya Mkenya Lucy Karimi (2:28:36) na Muethiopia Aberu Zennebe (2:29:07).