• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Kocha Sam Allardyce abanduka kambini mwa Leeds United

Kocha Sam Allardyce abanduka kambini mwa Leeds United

Na MASHIRIKA

KOCHA Sam Allardyce ameagana na Leeds United baada ya kipindi kifupi kilichomshuhudia akisimamia michuano minne kukamilika kwa waajiri wake kuteremshwa ngazi kwenye Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).

Allardyce, 68, aliongoza Leeds kupoteza mechi tatu na kupiga sare moja tangu amrithi Javi Gracia mnamo Mei 3, 2023.

Leeds watarejea sasa kwenye Ligi ya Daraja ya Kwanza nchini Uingereza (Championship) baada ya kunogesha EPL kwa miaka mitatu.

“Imekuwa fahari tele kuwa kocha wa Leeds United, kikosi kinachojivunia mashabiki wengi wenye matarajio makuu; na ambao kwa kweli wanastahili kuwa katika EPL,” akasema Allardyce.

“Katika kipindi hiki cha taaluma yangu, nisingependa kuendelea kuwa kocha wa kujifunga kwenye miradi mirefu. Hata hivyo, natakia klabu kila la heri katika Championship ili irejee katika EPL,” akasema.

Afisa Mkuu Mtendaji wa Leeds, Angus Kinnear, alisema: “Tunamshukuru Sam kwa ukakamavu wa kukubali kujiunga nasi na kufanya kila lililowezekana ndani ya uwezo wake kuokoa chombo chetu.”

Leeds wameahidi kutoa tangazo kuhusu kocha wao mpya katika kipindi cha wiki chake zijazo.

Allardyce ndiye kocha wa tatu wa kushikilia mikoba kwa muda mfupi kambini mwa Leeds msimu wa 2022-23 ulioanza chini ya Jesse Marsch aliyewaongoza kusalia ligini mwishoni mwa msimu wa 2021-22. Hata hivyo, Marsch alitimuliwa chini ya mwaka mmoja wa kuhudumu mnamo Februari 6, 2023.

Ingawa Gracia aliinua kikosi na kukiondoa ndani ya mduara wa vikosi vitatu vya mwisho, kichapo cha 4-1 kutoka kwa Bournemouth kilitosha kutimuliwa kwake pamoja na mkurugenzi wa soka, Victor Orta. Kuondoka kwao kulipisha Allardyce na msaidizi wake Karl Robinson.

Allardyce, ambaye hakuwahi kudhibiti mikoba ya kikosi chochote tangu ateremshwe ngazi ligini kwa mara ya kwanza kabisa akidhibiti mikoba ya West Bromwich Albion mnamo 2020-21, aligonga vichwa vya habari wakati wa hotuba yake ya kwanza kambini mwa Leeds kwa kujilinganisha na wakufunzi wazoefu Pep Guardiola (Manchester City), Jurgen Klopp (Liverpool) na Mikel Arteta (Arsenal).

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Pigo kwa Uhuru na Kioni, msajili wa vyama vya kisiasa...

Florence Diamond League: Chepng’etich afuta rekodi ya...

T L