• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 9:01 PM
Kuwasili kwa Moises Caicedo kwawasisimua mashabiki wa Chelsea

Kuwasili kwa Moises Caicedo kwawasisimua mashabiki wa Chelsea

Na MASHIRIKA

CHELSEA hatimaye walifaulu kumsajili kiungo mzoefu wa Brighton, Moises Caicedo, kwa Sh18.2 bilioni japo ada hiyo inatarajiwa kufikia Sh20.9 bilioni, ambayo ni rekodi mpya ya Uingereza.

Hadi kufikia mwisho wa wiki iliyopita, Liverpool walikuwa radhi kufungulia mifereji yao ya pesa na kumsajili Caicedo, 21, kwa Sh20.2 bilioni.

Hata hivyo, matamanio ya nyota huyo raia wa Ecuador yalikuwa kujiunga na Chelsea ambao sasa watavunja rekodi ya Uingereza mara mbili mwaka huu wa 2023 baada ya kumsajili kiungo Enzo Fernandez wa Argentina kwa Sh19.5 bilioni kutoka Benfica ya Ureno mnamo Januari 2023.

Caicedo alijiunga na Brighton mnamo Februari 2021 baada ya kuagana na Independiente del Valle ya Ucuador kwa Sh728 milioni pekee.

Sasa amekuwa sajili wa nane wa Chelsea muhula huu baada ya Axel Disasi, Christopher Nkunku, Nicolas Jackson, Lesley Ugochukwu, Angelo Gabriel, Robert Sanchez na Diego Moreira.

Chelsea walioambulia sare ya 1-1 dhidi ya Liverpool katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) ugani Stamford Bridge mnamo Agosti 13, 2023, tayari wameagana na Mateo Kovacic, Edouard Mendy, Kalidou Koulibaly, Kante, Mason Mount, Kai Havertz, Christian Pulisic, Ruben Loftus-Cheek, Ethan Ampadu, Pierre Emerick-Aubameyang, Abdul Rahman Baba na Cesar Azpilicueta.

Isitoshe, wamemtuma kipa Kepa Arrizabalaga hadi Real Madrid kwa mkopo wa msimu mmoja baada ya kumsajili Sanchez kwa mkataba wa miaka saba kutoka Brighton.

Jaribio lao la kujinasia Romeo Lavia, 19, kutoka Southampton kwa Sh10 bilioni limegonga mwamba baada ya Liverpool kuweka mezani Sh10.9 bilioni kwa ajili ya kiungo huyo raia wa Ubelgiji.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO 

  • Tags

You can share this post!

Jeraha la paja kumweka De Bruyne mkekani kwa miezi minne

Uhispania kusubiri mshindi wa mechi kati ya Uingereza na...

T L