NA MASHIRIKA
KOCHA wa Liverpool, Jurgen Klopp, amesema kikosi chake kipo tayari kuvuruga juhudi za vinara Arsenal kubeba Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu, watakapowakaribisha ugani Anfield siku ya Jumapili.
Hii ni baada ya Liverpool kuagana 0-0 na Chelsea katika gozi la EPL uwanja wa Stamford Bridge, London, mnamo Jumanne usiku.
Mjerumani huyo alipumzisha vigogo kadha katika mechi hiyo akitupia jicho mechi ya Jumapili jioni, ambapo anatazamiwa kuunda kikosi kikali kitakachopambana na Arsenal. Mshambuliaji matata Mohamed Salah, mabeki Trent Alexander-Arnold, Andy Robertson pamoja mlinzi mahiri Virgil van Dijk ni miongoni mwa vigogo walioanzia benchi katika mechi hiyo ambayo Liverpool walifanya mashambulizi butu.
“Tunatarajia upinzani mkali Jumapili, lakini tumejipanga kushinda siku hiyo. Tunaifahamu vizuri Arsenal ambayo kwa sasa inashikilia uongozi wa ligi,” alitanguliza Klopp baada tu ya sare ya Jumanne.
“Lakini pia sisi tunapigania kumaliza ligi katika nafasi nzuri. Wachezaji wangu wamejipanga kikamilifi kwa ajili ya pambano hilo,” akaongeza.
Alitoa onyo kwa vinara kwamba wataelekeza nguvu zao zote kwa mechi hiyo ikizingatiwa watakuwa nyumbani Anfield. Katika mechi ya Jumanne, Chelsea walicheza vizuri dakika zote 90 lakini mashambulizi yao hayakufua dafu, huku teknolojia ya VAR ikifuta mabao yao mawili kutoka kwa Reece James na Kai Havertz.
Fowadi mpya Joao Felix alionesha mbwembwe za kupepeta boli hapa na pale ila kila mara aliishia kuchanganyikiwa kutoa pasi za kuzaa bao. Hata hivyo, ilikuwa raha kwa mashabiki kumuona kiungo mkabaji N’Golo Kante uwanjani baada ya takriban miezi minane nje sababu ya jeraha. Kante alicheza kwa makini kabla kuondolewa dakika ya 70 akavute pumzi, ikizingatiwa ilikuwa mechi yake ya kwanza tangu Agosti 2022. Kocha Enrique kutua Chelsea? Chelsea walicheza chini ya uongozi wa kocha mshikilizi Bruno Saltor baada Graham Potter kupigwa kalamu Jumapili iliyopita.
Mkufunzi wa zamani wa Barcelona na timu ya taifa ya Uhispania, Luis Enrique, anaongoza orodha ya makocha saba wanaochambuliwa kuwa mrithi wa kudumu wa Potter – ambayo pia inajumuisha Mauricio Pochettino zamani wa Tottenham Hotspur katika EPL na Julian Nagelsmann zamani wa Bayern Munich nchini Ujerumani.
Hiyo jana, vyombo vya habari Uingereza viliripoti Enrique, 52, kuwasili jijini London kwa gumzo zaidi la kina na Chelsea baada ya majadiliano ya awali kufana. Kwenye mechi zingine za Jumanne usiku ligini EPL, wageni Aston Villa walipepeta Leicester City 2-1 ugani King Power; Brighton wakanyanyasa Bournemouth 2-0 kwao uwanjani Vitality; nao wenyeji Leeds wakafinya wanyonge wenzao Nottinham 2-1 ugani Elland Road.