• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 10:50 AM
Leteni hao Uganda, chipukizi wa Kenya wafoka baada ya kuminya Tanzania

Leteni hao Uganda, chipukizi wa Kenya wafoka baada ya kuminya Tanzania

NA JOHN ASHIHUNDU

Kenya Juniors Stars watakutana na Uganda katika fainali ya Cecafa U-18 itakayochezewa Jomo Kenyatta International Stadium, Kisumu.

Junior Stars walifuzu kwa fainali hizo Jumanne, Desemba 5, 2023 baada ya kuibwaga Tanzania 4-3 kupitia kwa mikwaju ya penalti baada ya timu hizo kutofungana katika muda wa kawaida wa dakika 90, pamoja na muda wa ziada wa dakika 30.

Kwa jumla, mechi hiyo ilichezwa kwa dakika 120 kabla ya mshindi kuamuliwa kupitia kwa matuta hayo, ambapo Kenya ilifunga kupitia kwa Collins Ochieng’, Amos Wanjala, Humphrey Aroko na Syphas Owuor, wakati penalti ya Stanley Omondi ikinyakwa na kipa Athony Mpemba wa Tanzania.

Tanzania walipfunga penalti zao kupitia kwa Benjamin Ramadhan, Hijjah Lidah na Phales Mkude. Kipa Ibrahim Wanzala alizuia mkwaju wa Said Said kabla ya Sharif Wilson kupiga nje penalti yake.

Owuor aliyefunga penalti ya ushindi aliingizwa katika kipindi cha pili katika nafasi ya Louis Ingavi aliye masomoni nchini Amerika anakoimarisha kipaji chake cha soka katika chuo cha Montverde Academy.

Zaidi ya mashabiki 20,000 walihudhuria mechi hiyo ambayo pia ilihudhuriwa na watu mashuhuri akiwemo Waziri wa Michezo, Ababu Namwamba pamoja na viongozi wa soka nchini.

Wachezaji wa Tanzania walibaki wakisugua vichwa vyao baada ya mechi hiyo kumlizika, lakini watapata fursa nyingine kuwania nishani ya shaba watakapokutana na Rwanda katika mechi ya kupigania nafasi ya tatu.

Mara tu mechi hiyo ilipomalizika, mashabiki wa matabaka mbali mbali walimiminika uwanjani, barabarani mjini Kisumu katika sehemu nyingine kote nchini kuusherehekea ushindi huo.

“Tumefurahia kushinda na sasa tumebakia na deni la kushinda Uganda na kubeba ubingwa Ijumaa mbele ya mashabiki wetu wa nyumbani,” alisema kocha Salim Babu aliyekiri kwamba walipata upinzani mgumu dhidi ya Tanzania.

Uganda walifuzu baada ya kushinda Rwanda kwa bao lililofungwa na Abubakar Mayanja, ambalo limezua utata miongoni mwa mashabiki kwa madai kwamba Mayanja alipachika bao hilo wavuni akiwa ameotea.

  • Tags

You can share this post!

Kuna ubaguzi katika misaada ya El Nino, mbunge Mishi Mboko...

Jinsi ya kuandaa mlo bora bila kutumia mafuta

T L